1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MANILA : Kimbunga chauwa mamia

2 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCnQ

Maafisa nchini Ufilipino wako mbioni kukabiliana na maafa yaliosababishwa na kimbunga Durian ambacho kimeuwa mamia ya watu.

Ofisi ya Ulinzi wa Raia imesema watu 208 wamekufa na 261 hawajulikani walipo katika eneo la vijijini la Bicol licha ya kwamba idadi ya vifo inaweza kuongezeaka wakati waokowaji wakiendelea kuopowa maiti kutoka vifusi vya maromoko ya ardhi yaliosababishwa na kimbunga hicho kikali kabisa.

Takriban watu 30,000 wameachwa bila ya makaazi na jamii nzima za vijijini zimetengwa kutokana na kukatika kwa umeme na mawasiliano ya simu ,kusombwa kwa madaraja na kuzibwa kwa barabara.

Kimbunga hicho Durian hapo jana kimeingia kwenye Bahari ya China Kusini baada ya kuwaathiri karibu watu nusu milioni nchini Ufilipino na kasi yake inatarajiwa kupunguwa kwa kugeuka kuwa dhoruba ya kiangazi kabla ya kupiga Vietnam hapo Jumatatu.