1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Malema atimuliwa rasmi ANC

25 Aprili 2012

Chama kinachotawala Afrika Kusini ANC kimemfukuza rasmi uanachama aliyekuwa kiongozi wa Umoja wa Vijana, Julius Malema baada ya kamati ya rufaa kutupilia mbali maombi yake.

https://p.dw.com/p/14ke6
Julius Malema akitafakari jambo enzi zake akiwa Rais wa Umoja wa Vijana wa ANC
Julius Malema akitafakari jambo enzi zake akiwa Rais wa Umoja wa Vijana wa ANC.Picha: picture-alliance/dpa

Maamuzi haya yanakamilisha miezi tisa ya hatua za kinidhamu ndani ya chama hicho kulishughulikia tatizo hilo, ambayo limemalizikia kwa kumuondoa kabisa Malema katika majukwaa ya siasa ya ANC.

Maamuzi ya kamati ya ANC iliyoketi jana, ambayo Malema aliitegemea kumuhurumia, ndiyo ya mwisho na hakuna dalili za yeye kupokelewa na chama kingine cha siasa.

Msimamo mkali wa Malema

Kiongozi huyo kijana wa miaka 31, ambaye ameonekana kuwa na ushawishi kwa vijana wengi, analaumiwa kwa misimamo mikali na matamshi yake ya wazi ambayo yamemgharimu sasa uanachama wake.

Tabia za Malema zilioneka kuwa kero kubwa kwa viongozi wa ANC, ambao kwa sasa wanajiandaa na mkutano mkuu uliopangwa kufanyika disemba mwaka huu na kumchagua kiongozi wa chama hicho ambapo kwa desturi ndiye atakayegombea pia urais wa tiketi ya ANC katika uchaguzi ujao mwaka 2014 nchini humo. Rais Jacob Zuma anatarajiwa kugombea tena wadhifa huo.

Malema anasema Rais Zuma ni mtawala wa kiimla, kauli ambayo aliirudia hata alipoulizwa na kamati hiyo iliyokuwa na maamuzi ya mwisho.

Tuhuma zingine zinamkabili

Akisema hadharani bila woga Malema, kijana kutoka jimbo masikini kabisa la Limpopo aliwavutia vijana wengi wa taifa hilo hasa baada ya kugusia tafauti baina ya matajiri na masikini na ubaguzi wa rangi katika nchi hiyo iliyomaliza utawala wa weupe wachache mwaka 1994 na kumuingiza madarakani Rais wa kwanza mweusi wa ANC Nelson Mandela.

Rais wa Afrika Kusini Jaco Zuma
Rais wa Afrika Kusini Jaco ZumaPicha: picture-alliance/dpa

Bado anachunguzwa na idara ya mapato ya Afrika Kusini kwa tuhuma nyingi, miongoni mwazo ni maisha yake ya anasa.

Maamuzi hayo yaliwakumba pia viongozi wengine sita wa umoja wa vijana wa chama hicho ambao walikuwa wanamuunga mkono Malema kwa karibu.

Nafasi ya kukata rufaa mahakama

Mwaka 2010 Julius Malema alipewa adhabu kwa kumuita mwandishi wa habari mmoja kuwa ni kibaraka alipomshurutisha kutoka nje ya ukumbi wa mkutano katika jengo la umoja wa vijana la ANC akidai kuwa jengo hilo sio chumba cha habari ambapo kila mtu anajizungumzia tu, akimalizia kuwa jengo hilo ni la kimapinduzi.

Rais wa Kwanza wa Afrika Kusini Nelson Mandela akiwa na Askofu Desmond Tutu.
Rais wa Kwanza wa Afrika Kusini Nelson Mandela akiwa na Askofu Desmond Tutu.Picha: picture-alliance/dpa

Malema anapingana vikali na mwenyekiti wa sasa wa ANC huku kumfukuza huko kukitazamwa kama kuondoa ushawishi wa kumpinga Jacob Zuma katika mkutano ujao wa chama hiki ambapo kura zitapigwa.

Pia kunatarajiwa wajumbe kupitisha sera za muelekeo wa ANC na kuamua kama Jacob Zuma kuendelea kuwa mwenyekiti wao au la.

Lakini nafasi ya kukata rufaa anayo kwa kupeleka maombi hayo katika mahakama za Afrika Kusini.

Mwandishi: Adeladius Makwega/DPAE

Mhariri: Mohammed Khelef