1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Malawi yapitisha muswada wa taarifa sekta ya madini

Sylvia Mwehozi
25 Januari 2017

Hivi karibuni Malawi imepitisha muswada wa sheria kuhusu upatikanaji wa taarifa ambao utazisaidia jamii zilizoathirika na sekta ya madini kupata taarifa za masuala yanayohusiana na mazingira, afya na hatari za usalama. 

https://p.dw.com/p/2WMJe
Peter Mutharika wird neuer Präsident von Malawi 31.05.2014
Picha: picture-alliance/AP Photo

Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch kwa kushirikiana na mtandao unaotetea Maliasili nchini Malawi umetoa taarifa hiyo. 

Bunge la Malawi lilipitisha muswada huo kwa kuufanyia mabadiliko mnamo Desemba 14 mwaka jana na tayari umepelekwa kwa Rais Peter Mutharika ambapo unasubiriwa kusainiwa kabla ya kuanza utekelezaji.

Mtandao unaotetea Maliasili nchini Malawi umekuwa ukitetea kwa zaidi ya muongo mmoja kwa ajili ya upatikanaji wa taarifa ambazo zitasaidia jamii kuweza kufanya maamuzi na kuwawajibisha viongozi katika sekta hiyo ya madini.

Sheria hiyo mpya inamaanisha kwamba wananchi katika jumuiya za madini Malawi watapaswa kuwa na uwezo wa kupata taarifa muhimu ambazo wanazihitaji katika kulinda maisha yao alisema Katharina Rall, mtafiti katika shirika la Human Rights Watch, akitoa wito kwa rais wa nchi hiyo kutia saini muswada huo.

Afrika Kongo Goldgewinnung Tagebau
Shughuli za uchimbaji madini Picha: GettyImages/R. Olson

Katika ripoti ya mwaka uliopita, Human Rights Watch ilisema familia zinazoishi karibu na maeneo ya uchimbaji mkaa na Uranium wanakabiliwa na matatizo mengi yakiwemo ya maji, chakula na malazi na kwamba familia hizo zimeachwa gizani kuhusu athari za kiafya na nyinginezo kutokana na shughuli za uchimbaji zinazofanyika.

Ripoti hiyo ilibainisha kwamba Malawi inakosa ulinzi wa kutosha ili kuhakikisha kwamba juhudi za maendeleo zinakwenda sambamba na ulinzi wa haki za jamii zinazozunguka maeneo hayo na kwamba serikali imekuwa na uangalizi dhaifu na kukosekana kwa taarifa kunawafanya wananchi kutokuwa salama.

Wananchi katika jamii za migodi na mashirika yasiyo ya kiserikali nchini humo walisema kamba walishindwa kupata taarifa za kutosha kuhusu shughuli zilizopangwa za uchimbaji na hatari zitokanazo na kuchochea  wasiwasi kuhusu magongwa ya kupumua na atahri nyingine za kiafya na mazingira. Serikali ya Malawi imeliambia shirika la Human Rights Watch kwamba inafuatilia athari za uchimbaji madini lakini haitoi taarifa za jamii zilizoathirika.

Peter Mutharika wird neuer Präsident von Malawi 31.05.2014
Rais wa Malawi Peter MutharikaPicha: AFP/Getty Images

Uamuzi wa bunge kupitisha muswada huo umepongezwa na jumuiya za migodini na kwamba huenda kutasaidia kuishinikiza serikali kutoa taarifa kuhusu shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi katika ziwa Malawi. Kossam Munthali ni mwenyekiti wa mtandao unaotetea Maliasili nchini humo, ambaye amesema kwamba bilaya kuwepo na taarifa kutoka upane wa serikali mashirika ya kiraia hayawezi kufahamu hatari muhimu zitokanazo na shughuli hizo. "Tunaamini kwa nguvu zote kwamba ili uchimbaji uwe endelevu wananchi wazawa wanapaswa kushiriki, wanapaswa kushirikishwa ili waweze kufuatilia kile wanachokimiliki. Katika hali ambayo hupati taarifa ni utani mkubwa. Kwahiyo pindi muswada huo utakaposainiwa itakuwa ni ukurasa mpya hususan kwamba watu watakuwa na uwezo wa kupata taarifa ambazo hutajwa kuwa ni za siri, tutakuwa na uwezo wa kuhoji pale mambo hayaendi sawa na uwezo wa kuhoji kuhusu mali zao", amesema Munthali. 

Ikiwa muswada huo utasainiwa kuwa sheria utawahakikishia wananchi wa Malawi wanakuwa na uwezo wa kuomba na kupata taarifa wanazohitaji kutoka mamlaka zote za serikali kama ilivyoanishwa katika katiba.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/HRW

Mhariri: Josephat Charo