"Makombora ya Scud yatumika Syria"
13 Desemba 2012Akithibitisha hilo afisa mmoja aliyezungumza kwa mashariti ya kutotaja jina lake, aliliambia shirika la habari la ufaransa AFP kwamba matukio ya makombora ya Scud yamidhihirika kutokeaa katika ardhi ya Syria. Awali mwandishi AFP huko upande wa kaskazini/magharibi mwa Syria alitoa taarifa ya kusikia miripuko mikubwa umbali wa kilometa 15, kutoka sehemu aliyokuwepo.
Msemaji wa wizara ya mambo ya nje wa Marekani Victoria Nuland alithibitisha kutokea mikasa ya kutumika silaha kali nchini Syria ingawa hakutaka kutaja aina ya silaha hizo zinazotumika. Lakini katika taarifa yake ya awali iliyochapishwa katika gazeti New York Times alitoa ahadi ya kuthibitisha kama utawala huo umetumia makombora ya Scud au la.
Hata hivyo hakujawa na taarifa za athari zozote, kutokana madai ya matumizi ya makombora hayo ambayo yalitumika sana wakati wa zama za Kisoviet, ambayo yalikuwa maarufu sana wakati wa vita vya Ghuba. Uwezo wa kusafiri kwa makombora hayo mafupi ya Scud, unategemea aina aina yake ambapo yanaweza kufyatuliwa kwa umbali wa kilometa 200 au zaidi ya hapo.
Taarifa ya kufyatuliwa makombora yanayoashiria kuwa Scud imethibitishwa pia na umoja wa kujihami wa NATO ambapo umesema wamebaini kufanyika mfulululizo wa aina ya makombora ya masafa mafupi yanayohisiwa kuwa Scud.
Aidha katika jitihada nyingine ya kuongeza shinikizo zaidi dhidi ya utawala wa Assad, jana mataifa ya kiarabu sambmba na magharibi yameutambua muungano wa waasi nchini humo kama chombo chenye kuwawakilisha raia wa taifa hilo.
Azimio hilo limepitishwa na kundi la matiafa linalojiiita "marafiki wa Syria" katika mkutano wao uliyofanyika mjini Morocco. Waziri wa Mambo ya Nje wa Morocco Saad Eddine El Othmani aliwaambia waandishi wa habari kwamba muungano huo wa waasi wameupa uwakilishi kamili wa raia wa Syria.
Mazungumzo hayo yalijikitia kuujdali mgogoro wa miezi 21 wa Syria uliyakutanisha wawakilishi kutoka matiafa 114, wakiwemo mawaziri wa mambo ya nje 60, Wapinzani wa Syria pamoja na asasi nyingine za kimataifa. Mataifa hayo marafiki ya Syria yamerejea wito wake wa kumtaka rais Assad ajiweke pembeni na kusisitiza kwamba utawala huo hauwezi kukwepa adhabu kutokana na kukiuka sheria ya kimataifa.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza William Hague ameita hatua ya kuongezeka mataifa kutambua upande wa uasi nchini Syria kama chombo chenye kuwakilisha wananchi kuwa ni maendeleo ya kweli.
Mwandishi: Sudi Mnette
Mhariri: Yusuf Saumu