1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Majeshi ya Afghanistan yaudhibiti mji mkuu

16 Aprili 2012

Afghanistan imeeleza kwamba majeshi yake yamefanikiwa kuudhibiti tena mji wa Kabul uliokuwa umeshambuliwa na waasi wa kundi la Taliban. Shambulizi hilo lilikuwa kubwa zaidi kutokea Kabul katika kipindi cha miaka 10.

https://p.dw.com/p/14eWg
Askari wa NATO nchini Afghanistan
Askari wa NATO nchini AfghanistanPicha: Reuters

Vikosi vya serikali ya Afghanistan ndivyo vilivyoongoza operesheni hiyo ya kuurudisha mji huo mkuu mikononi mwake, lakini msemaji wa jeshi la Jumuiya ya Kujihami ya NATO, amesema kwamba walitoa msaada kwa vikosi hivyo baada ya kuombwa kufanya hivyo. Watu 47 waliuwawa nchini Afghanistan katika mashambulizi yaliyofanywa na wapiganaji wa kundi lenye msimamo mkali wa Kiislamu, Taliban. Mashambulizi hayo yalifanyika katika mji mkuu Kabul na miji mingine mitatu kwa muda wa masaa 18.

Katika mkutano na waandishi wa habari, waziri wa mambo ya ndani wa Afghanistan, Bismillah Mohammadi alieleza kwamba mbali na kusababisha vifo vya watu 47, shambulizi la wataliban liliwajeruhi pia watu 65, 40 kati yao wakiwa maafisa wa usalama na 25 raia wa kawaida. Mohammadi alisema kwamba waasi 16 ndio waliofanya mauaji mjini Kabul. "Walipokuwa wakiingia mjini walikuwa wamevaa hijabu . Waliweka maua katika gari lao kuashiria kwamba wanakwenda kwenye sherehe," alieleza waziri huyo.

Waziri wa mambo ya nje wa Afghanistan, Bismillah Mohammadi
Waziri wa mambo ya nje wa Afghanistan, Bismillah MohammadiPicha: picture-alliance/dpa

NATO yaisifu Afghanistan

Milio ya risasi ilianza kusikika Jumapili mchana katika miji ya Kabul, Jalalabad, Gardez na Logar. Kulitokea pia miripuko lakini baadaye wanajeshi wa Afghanistan walianza kujibu mashambulizi ambapo baadhi ya wapiganaji wa Taliban waliuwawa.

Kamanda wa jeshi la ISAF la kundi la kujihami la NATO, Jenerali John Allen, amewapongeza maafisa wa usalama wa Afghanistan kwa jinsi walivyopambana na waasi. "Walikuwa wamejipanga vizuri na kuongozwa vizuri na walitumia juhudi yao kulinda maisha ya raia wenzao," alisema Allen.

Kamanda wa majeshi ya ISAF, Jenerali John Allen
Kamanda wa majeshi ya ISAF, Jenerali John AllenPicha: dapd

Naye mkuu wa polisi wa mji wa Kabul, Jenerali Ayoub Salangi, ameeleza kwamba watu 35 walitekwa na waasi karibu na jengo la Bunge la Afghanistan lakini hata hivyo watu hao baadaye waliweza kuokolewa. Kwa mujibu wa mkuu wa polisi, ni mwanamke mmoja tu aliyejeruhiwa.

Ubalozi wa Ujerumani washambuliwa

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani, Guido Westerwelle, amelaani mapigano yaliyotokea Afghanistan na kuahidi kwamba nchi yake itaendelea kuyaunga mkono maendeleo yanayofanyika Afghanistan. "Tutaendelea kupambana na uasi wa magaidi," alisema Westerwelle. Tutaendelea kusaidia kujenga Afghanistan yenye amani na yenye mazingira mazuri ya kuishi. Licha ya kuwekewa vikwazo,tutaendeleza sera yetu ya kulikabidhi jukumu la usalama wa nchi kwa raia ." 

Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani, Guido Westerwelle
Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani, Guido WesterwellePicha: dapd

Ubalozi wa Ujerumani ni miongoni mwa majengo yaliyoshambuliwa katika mapigano yaliyoanza jana Jumapili. Hata  hivyo Westerwelle ameeleza kwamba hakuna mtu aliyejeruhiwa katika ubalozi huo. Wafanyakazi wote walipelekwa mahali penye usalama.

Mwandishi: Elizabeth Shoo/AFP/DPA

Mhariri: Mohammed Khelef