1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Majambazi wahadaa chipukizi Ivory Coast

Ramadhan Ali27 Machi 2007

Chipukizi 34 wahadaiwa na ajenti-bandia huko Ivory Coast kuletwa ulaya kucheza dimba na mwishoe wamalizikia mitaani Mali.Mashabiki 3 wauwawa Nigeria.

https://p.dw.com/p/CHcS

Baada ya changamoto za mwishoni mwa wiki za kuania tiketi za finali za kombe la Ulaya mwakani nchini Uswisi,timu kadhaa za ulaya zinarudi uwanjani jioni ya leo kwa duru nyengine.Ujerumani baada ya kuikomea Jamhuri ya Czech mabao 2:1 mjini Prague, hapo jumamosi, ina miadi leo na Denmark kwa mpambano wa kirafiki.

Si chini ya wachezaji 6 wa timu ya Eritrea waomba ukimbizi Angola.Polisi yaua mashabiki wa 3 Nigeria na chipukizi 34 kutoka Ivory Coast wahadaiwa na jambazi kuja Ulaya kucheza dimba na waishia kambini nchini Mali.

Chipukizi 34 kutoka Ivory Coast walioahidiwa siku moja watakuwa mastadi wa dimba huku Ulaya na dalali-bandia wamerudi nyumbani bila kutia mguu Ulaya .Shirika la Uhamiaji la kimataifa (IOM) liliripoti jana kwamba mkasa huo ni mmoja tu kati ya taitizo kubwa na lililo tapakaa chini kwa chini barani Afrika ambamo majambazi wanaojidai ni maargenti wanawahadaa vijana kuwaleta Ulaya kucheza kabumbu.

Wazee wa chipukizi hao wenye umri kati ya miaka 16-18 wanaoichezea timu ya vijana katika mtaa wa madongo poromoka nje ya Abidjan,wazee wao walihadaiwa kulipa kitita cha hadi dala 600 kila mmoja ili watoto wao wapatiwe nafasi ya kuzichezea klabu mashuhuri za Ulaya.

Badala yake vijana hao walisafirishwsa kimagnedo hadi nchi jirani ya Mali miezi 3 iliopita na huko wakagunduliwa na polisi kufuatia msako wakilala sakafuni katika nyumba moja ya mji wa Sikasso wakiwa na chakula kidogo.Ajenti huyo bandia na rais wa club hiyo ya dimba ya watoto hao wametiwa sasa nguvuni na wanakabili mashtaka ya uhalifu.

Na huko Angola mara tu baada ya Angola kuitimua nje Eritrea mwishoni mwa juma katika mpambano wa kuania tiketi za finali ya kombe la Afrika la mataifa mwakani nchini Ghana, wachezaji alao 6 wa timu ya taifa ya Eritrea wameukata na wameomba ukimbizi Angola.Majina ya wachezaji hao hayakufichuliwa na sasa wanahofia kuwa serikali ya Angola haitaitikia ombi lao .

Waeritrea waliojaribu kuikimbia nchi yao na kutofaulu adhabu imekuwa kifo nyumbani.tarakimu za wanaotafuta ukimbizi zilizochapishwa na shirika la wakimbizi la UM UNHCR zimeonesha muongezeko wa 59% kutoka Eritrea mwaka jana.

Huko Nigeria,mashabiki 3 wa dimba wameuliwa uwanjani na polisi baada ya kuzusha machafuko uwanjani wakati wa mpambano wa Ligi.Polisi aliewekwa kuulinda upande wa Enyimba ndie aliewafyatulia risasi na kuwaua mashabiki 3 pale machafuko yalipoanza.Mashabiki walihemkwa baada ya rifu Felicia Okwugba kutoa adhabu ya penalty dakika za mwisho za mchezo baina ya Enyimba na Akwa united huku Akwa ikiongoza kwa mabao 2:1.

Mashabiki hao walimuandama rifu huyo na kumlazimu rifu aliewekwa kuilinda enyimba kufyatua risasi.mashabiki hao waliachoma moto magari kadhaa yalioegeshwa uwanjani na kupambana na polisi.Siku ya pili yake jana jumatatu vijana waliokuwa na hasira waliingia mitaani wakiharibu mali na kuwasaka wanigeria watokao mashariki ya nchi hiyo-makao ya timu ya Enyimba.

Shetani wa mpira alao kwa sasa amepungwa huku ulaya na hasa katika mpambano wa leo wa kirafiki kati ya Ujerumani na Denmark.Kocha wa Ujerumani Joachim Loew, hajali matokeo ya mpambano wa leo kinyume na ule wa jumamosi dhidi ya Jamhuri ya Czech uliokuwa wa kuania tiketi ya finali za Kombe la Ulaya mwakani huko Uswisi. Leo ikiwa ni mechi ya kirafiki, ameamua kuteremsha timu ya majaribio huko Duisburg,Ujerumani.

Nahodha Michael Ballack amewekwa nje pamoja na mastadi kadhaa waliotamba jumamosi.Robert Enke anateremshwa leo uwanjani kwa mara ya kwanza kulinda lango badala ya Jens Lehmann –kipa wa Arsenal.Kevin Kuranyi, mtiaji wa mabao 2 dhidi ya Jamhuri ya Czech atakuwa tena uwanjani.

Katika medani ya riadha,mji wa Korea ya kusini wa Daegu, umechaguliwa huko Mombasa na shirikisho la riadha ulimwenguni-IAAF kuandaa mashindano ya ya ubingwa wa riadha wa dunia kwa mwaka 2011.Moscow zamu yake itakuwa 2013 kwa muujibu wa rais wa IAAF Lamine Diack wa Senegal.