1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mafuta bado kuinufaisha Chad

Sekione Kitojo17 Oktoba 2013

Wakosoaji wanamueleza rais Idriss Deby wa Chad kwa maneno machache. Wapinzani wasiotakiwa nchini humo hunyamazishwa ama kununuliwa, na anafanya hivyo kwa kutumia mapato yatokanayo na mafuta.

https://p.dw.com/p/1A0bu
Rais Idriss Deby wa Chad akishikana mikono na majenerali wa Chad katika jeshi la nchi hiyo lililoko Mali.
Rais Idriss Deby wa Chad akishikana mikono na majenerali wa Chad katika jeshi la nchi hiyo lililoko Mali.Picha: STR/AFP/Getty Images

Kwa nje lakini rais Deby anajionesha kuwa ni mtu safi kabisa. Jeshi kama sehemu ya msaada katika masuala ya dharura , linatatua mizozo pamoja na wanamgambo katika maeneo ya magharibi na kati katika bara la Afrika. Hali inakuwaje katika ukandamizaji wa Deby ndani ya nchi hiyo na nguvu za kijeshi vikiunganishwa?

Katika orodha ya mataifa duniani Tchad licha ya kupata mapato makubwa kutokana na mafuta iko katika nafasi dhaifu sana. Katika kielelezo cha Umoja wa Mataifa kuhusu nchi zinazoendelea Chad iko katika nafasi ya 184 kutoka mataifa 187, ambapo nchi ambazo bado hazijapiga hatua kubwa katika maendeleo ni Msumbiji, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Niger.

Pamoja na kuwa na utajiri wa mafuta, Chad bado ina miundombinu duni.
Pamoja na kuwa na utajiri wa mafuta, Chad bado ina miundombinu duni.Picha: Christof Krackhardt

Ukandamizaji wa haki za binaadamu
Matarajio ya watu kuishi nchini Chad ni karibu miaka 50, ambapo kila mtu mzima wa tatu anaweza kusoma na kuandika na asilimia 62 ya watu milioni 11 nchini Chad wanaishi kwa kutumia chini ya euro moja kwa siku. Haki za binadamu hukandamizwa, wapinzani hunyamazishwa, anasema Martin Petry, mshauri wa maendeleo wa kujitegemea na anaeifahamu Chad tangu miaka kadha iliyopita.

"Nchini Chad kama ilivyokuwa hapo kabla wapinzani wanakamatwa na kufanyiwa vitendo vya kikatili. Kumekuwa na matukio kadha ya kukamatwa , rushwa ndogo ndogo ni nyingi , na pia matumizi mabaya ya madaraka ya polisi, na wanamgambo. Iwapo mtu nchini Chad atanyimwa kuhusu haki yake, ni vigumu kuidai na kuipata tena," anasema Petry.

Rais Idriss Deby ameitawala nchi hiyo tangu mwaka 1990 na yuko madarakani sasa kwa muda wa miaka 23. Katika muda huu wa kuwapo madarakani , amekuwa akitofautiana kidogo sana na viongozi wengine wa mataifa ya Afrika kama vile Teodoro Obiang Nguema wa Guinea ya Ikweta , Jose Eduardo dos Santos wa Angola ama Robert Mugabe wa Zimbabwe.

Wafanyakazi wa Chad wakielekeza bomba la mafuta katika kisima cha Doba kusini mwa nchi hiyo.
Wafanyakazi wa Chad wakielekeza bomba la mafuta katika kisima cha Doba kusini mwa nchi hiyo.Picha: AP

Fedha za mafuta zaimarisha uwezo wa jeshi
Jeshi la Chad ndilo jeshi lililopata mafunzo mazuri zaidi na lenye vifaa vya kisasa kabisa katika bara la Afrika kusini mwa jangwa la Sahara. Hii imetokana na mapato ya mafuta ambayo yameanza kupatikana miaka kumi iliyopita. Helga Dickow , mtaalamu wa Chad kutoka taasisi ya Arnold-Bergstraesser katika chuo kikuu cha Freiburg nchini Ujerumani anasema.

"Fedha za mafuta zimemsaidia kujenga nguvu za kijeshi nje ya nchi . Chad kwa sasa ina jeshi lenye vifaa vya kisasa kabisa kusini mwa jangwa la Sahara. Kwa siasa za ndani lakini fedha za mafuta zimemjengea Deby madaraka makubwa ya kisiasa. Utawala wake una udhibiti kamili wa fedha zote za mafuta na unaweza kutumia fedha hizo kwa ajili ya kampeni za uchaguzi. Upendeleo na kuwatuliza wapinzani wa kisiasa ni mbinu kuu kama ilivyokuwa zamani."

Deby huwatumia watu anaowapendelea kuwakandamiza baadhi ya watu wengine. Hawa wanajulikana kutokana na kushirikiana kwa karibu na utawala huo. Wapinzani wa kisiasa wanavutwa upande wake kwa kuwapa nyadhifa za heshima na kuweza kuwaingiza katika mfumo wake wa utawala. Fedha nyingi hutumiwa nchini Chad katika ujenzi wa madaraka yake, lakini ni fedha chache zinazokwenda katika kupambana na umasikini ama ujenzi wa miundo mbinu.

Jeshi ambalo limeimarishwa kutokana na fedha za mafuta analitumia Deby kupata nafasi ya kutambulika kimataifa. Januari mwaka huu (2013)kwa mfano wakati rais wa Ufaransa Francois Hollande alipopeleka vikosi vya jeshi nchini Mali yeye aliweka tayari wanajeshi karibu 2,400 kutoka Chad .

Ramani ya Chad ikionyesha maeneo yaliko mafuta.
Ramani ya Chad ikionyesha maeneo yaliko mafuta.Picha: DW

Sera ya mambo ya kigeni ni muhimu
Akipambana na waasi wa Kiislamu na makundi ya kigaidi Deby anajaribu kupata kutambulika katika medani ya kimataifa na amefanikiwa katika suala moja. Chad inapata ukosoaji mdogo kuhusiana na siasa zake za ndani kuhusiana na uendeaji kinyume haki za binadamu.

Ni kwa kiasi gani mkakati huu wa Deby unavyofanyakazi, unaonekana pia katika mtazamo wa bara la Afrika binafs , kwamba sera za mambo ya kigeni ni muhimu , kama inavyooneshwa katika makubaliano yaliyofikiwa na Umoja wa Afrika, kwamba wanataka kuiunga mkono Chad katika kuwania nafasi ya kuwa mwanachama ambae si wakudumu katika baraza la usalama la Umoja wa mataifa katika mwaka 2014 / 15.

Mwandishi : Köpp, Dirke / ZR / Sekione Kitojo
Mhariri: Josephat Charo