1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mafuriko yaathiri nchi nyingi barani Afrika

Jane Nyingi27 Septemba 2007

Wakulima nchini Ghana wamepoteza mazao yao mashambani kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa

https://p.dw.com/p/CHjB
Bendera ya taifa la Ghana
Bendera ya taifa la Ghana

Tulimuomba Mungu atufungulie mbingu lakini haya siyo tuliyoyategemea, nimekwisha mimi ni nani atakae nifa fedha za kuanzisha maisha mapya, hayo ni mtamshi ya Peter Nayoon akiuliza huku akionyesha kidole mahala palipokuwa na shamba lake la viazi vikuu, mkulima huyo kutoka Gushiegu eneo la kaskazini mwa Ghana likiwa ni moja kati ya maeneo yaliyokumbwa na mafuriko barani Afrika katika wiki chache zilizopita.

Ukame wa muda mrefu uliofuatiwa na mafuriko makubwa nchini Ghana umeathiri eneo zima la nchi hiyo kiasi cha kufikia kufungwa bwawa linalozalisha umeme la Akosombo lililoko kusisni mashariki mwa Ghana.

Bwawa hilo daima limekuwa likipokea mtiririko wa maji kutoka kaskazini mwa mto Volta. Hali ilibadilika mwishoni mwa mwezi Agosti wakati mvua kubwa ziliponyesha katika maeneo ya kaskazini na maeneo ya juu ya magharibi.

Mvua hizo kwanza zilifurahiwa na familia ambazo zilikuwa zinakabiliwa na hali ngumu ya ukame lakini zilibadilika na kuwa janga hadi kuzilamizisha familia kuyahama makaazi yao.

Takriban watu laki mbili na elfu hamsini wamepoteza makaazi yao hayo. ni kwa mujibu wa naibu waziri wa habari wa Ghana Frank Agyekum.

Bibi Joana Seini mama mwenye watoto wawili amesema kwamba alilazimika kuwalisha watoto wake majani aliyoyachuma nyuma ya nyumba yake iliyoharibiwa na mafuriko na kutumia maji yaliyojaa tope kwa kunywa.

Alhassan Samari waziri wa jimbo la kaskazini amesema kuwa, takriban ekari mia moja na moja za mashamba ya viazi vikuu zimesombwa na mafuriko.

Amefahamisha kwamba wilaya ya Saboba-Cheroponi katika jimbo la kaskazini imepoteza ekari 500 za mpunga, ekari mia moja na sitini za maharagwe, ekari mia sita na kumi na moja za mahindi na ekari mia moja na arobaini na tisa za njugu karanga.

Shirika la chakula duniani la umoja wa matiafa WFP limesema kuwa hadi sasa takriban watu elfu sabini na tano nchini Ghana wanahitaji kwa dharura msaada wa kibinadamu ikiwa ni pamoja na chakula, nguo, blankenti, vyombo, vyandarua, madawa ya kusafisha maji, na mitumbwi, shirika hilo limetoa tangazo hilo kwenye tovuti yake.

Maeneo yaliyoathirika yalitembelewa na wawakilishi wa mashirika ya kutoa misaada.

Watoto katika maeneo yaliyoathirika na mafuriko hawataweza kuendelea na masomo yao kutokana na shule kadhaa kuharibiwa na mafuriko hayo amesema bibi Yasmin Hague muwakilishi wa mfuko wa umoja wa matiafa unaosimamia watoto.

Bibi Hague ameelezea wasiwasi wake kuhusu kuzuka magonjwa yanayosababishwa na maji machafu, ameitolea mwito serikali ya Ghana kukabiliana na hofu hiyo kabla ya kutokea mkurupuko wa maradhi.

Mafuriko yamelikumba bara zima la Afrika, shirika la chakula la WFP limesema huenda watu milioni moja nukta tano wamegeuka wahanga wa mafuriko katika muda wa wiki chache za hivi karibuni.

Naibu waziri wa habari wa Ghana Frank Agyekum amesema hali nchini mwake imekuwa mbaya zaidi kutokana na kufunguliwa mifereji ya mabwawa kutoka nchi jirani ya Burkina Faso.

Afisa wa ubalozi wa Burkinabe nchini Ghana amethibitisha madai hayo lakini akatetea hatua ya serikali yake kwa kusema kuwa iwapo mfereji wa bwawa la Bagre usingefunguliwa basi bwawa hilo lingekabiliwa na hatari.

Waziri Agyekum amesema mafuriko hayo ni kwa sababu ya mabadiliko ya hali ya hewa duniani.