1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mabalozi wa Ulaya waahidi kuwasaidia wakimbizi Nyarugusu

2 Juni 2021

Mabalozi sita kutoka Umoja wa Ulaya na Uingereza nchini Tanzania wako ziarani katika kambi za wakimbizi magharibi mwa Tanzania, kuhakikisha kuwa wakimbizi wanapata huduma na ulinzi kadiri ya matakwa ya Umoja wa mataifa.

https://p.dw.com/p/3uMtx
Tansania Nyarugu Camp Regine Hess, Alkadiy Leybovskiy und Peter Van Acker
Kutoka kushoto ni Balozi Regine Hess wa Ujerumani, Bw. Alkadiy Leybovskiy (Afisa mkuu wa makazi -UNHCR) na Peter Van Acker Balozi wa Ubelgiji wakisikiliza maoni ya wakimbizi wa kambi ya Nyaurugusu, mkoani Kigoma, Tanzania, Juni 02, 2021.Picha: Prosper Kwigize/DW

Mabalozi hao ni pamoja na Balozi wa Ujerumani Bi Regine Hess, Balozi wa Uholanzi Bw. Jeroen Verheul, Balozi wa Denmark Bw. Mette Nirgaard, Balozi wa Uswiss Bw. Didier Chassot, Balozi Ubelgiji Bw. Peter van Acker na Balozi wa Uingereza David Concer.

Katika ziara hiyo wakimbizi wamelalamikia viongozi hao kwa kutoa misaada isiyokidhi mahitaji hususani chakula na kuni za kupikia pamoja na huduma nyingine za kijamii.

Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania Bi. Regine Hess ametumia fursa hiyo kuutaarifu umma wa wakimbizi kuwa Ujerumani itaendelea kutoa misaada mbalimbali ikiwemo udhamini wa elimu ya juu, afya na chakula kupitia mashirika yanayohudumia wakimbizi ya UNHCR, WFP, IRC na Save the Children.

Tansania Nyarugu Camp Safi Apelee
Mwakilishi wa Vijana Bi. Safi Apelee akiwasilisha hoja za vijana kwa mabalozi.Picha: Prosper Kwigize/DW

Waiomba EU kuongeza misaada

Pamoja na kuzishukuru serikali ya Tanzania, UN na Umoja wa Ulaya, wakimbizi wa Burundi na DRC wameungana na mweyekiti wa kambi ya Nyarugusu Bi. Abilola Angelique kuomba Umoja wa Ulaya utafakari kuongeza misaada hasa ya chakula ambacho kimepunguzwa kwa zaidi ya asilimia 32 na hivyo kusababisha adha na njaa kwa familia.

Soma pia: Ujerumani yasaidia utunzaji mbuga za wanyama Tanzania

Changamoto nyingine zilizotajwa na wakimbizi hao hasa vijana ni ukosefu wa ufadhili wa elimu, zana za michezo, kufutwa kwa siku ya vijana kwa wakimbizi na uhuru mdogo wa kutoka nje ya kambi kwa ajili ya kutafuta mahitaji mbalimbali ikiwemo chakula.

Pamoja na maeneoo mengine mabalozi hao wametembelea kituo cha watoto kinachosimamiwa na shirika la Save the Childreni kwa ufadhili wa serikali ya Ujerumani kupitia shirika la maendeleo la Ujerumani GIZ ambapo watoto hufundishwa michezo mbalimbali pamoja na stadi za maisha.

Tansania Nyarugu Camp Regine Hess
Balozi wa Ujerumani Regine Hess akifurahia jambo pamoja na watoto na watumishi wa shirika la Save the Children katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu.Picha: Prosper Kwigize/DW

Balozi Regine Hess ameridhishwa na maendeleo ya kituo hicho na kuahidi kuwa serikali ya Ujerumani itaendelea kutoa misaada ya kiutu ili kunusuru maisha ya watoto hao na wakimbizi kwa Ujumla

Nchi za Umoja wa Ulaya ndio wafadhili wakubwa wa misaada ya mahitaji mbalimbali kwa wakimbizi wa Burundi na DRC nchini Tanzania.

Mwandishi: Prosper Kwigize