1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maambukizi ya virusi vya Corona Afrika yaongezeka

Sekione Kitojo
20 Machi 2020

Mataifa ya Afrika yakiongozwa na Nigeria na Afrika kusini yameimarisha hatua za kupambana dhidi ya mripuko wa virusi vya Corona baada  ya bara hilo kurekodi kifo cha kwanza kutokana na ugonjwa huo.

https://p.dw.com/p/3ZnbN
Nigeria Lagos | Coronavirus | Temperaturmessung
Picha: DW/F. Facsar

Nigeria  imesema  inafunga  mashule  yote  nchini humo  na  kupunguza  shughuli  za  mikutano  ya  kidini  katika  mji wa  biashara  wa  Lagos  na  mji  mkuu  Abuja, wakati  Afrika  kusini , nchi  ambayo  ina uchumi  mkubwa  wa  viwanda  barani  humo, imechukua hatua ya kupunguza  riba kusaidia  makampuni  nchini humo. 

Körperlicher Abstand Schutzmassnahmen
Watu wakiwa wamekaa mbali mbali kuepuka maambukiziPicha: Reuters/K. Kyung-Hoon

Nigeria, nchi  ambayo  ina  wakaazi  wengi  zaidi  katika  bara  la Afrika na  ambayo  ina  wakaazi  wanaofikia  milioni 200, hadi  sasa imerekodi  idadi  ya  watu 12  walioambukizwa  virusi  vya  Corona na  unafuatia nchi  nyingine  katika  kuongeza  hatua  zake  za kupambana  na  virusi  hivyo. Serikali  ya  jimbo  la  Lagos imesema shule  katika  mji  huo  ambao  una  wakaazi  wapatao  milioni 20 zitafungwa  kuanzia  siku  ya  Jumatatu. Serikali ya  mji  huo imesema  kwamba  sasa  kuna  maambukizi  yanayotoka  ndani  ya mji  huo.

Idadi  ya  maambukizi  ya  virusi  vya  Corona  nchini  Afrika  kusini sasa  imepindukia   watu 200  leo  Ijumaa  wakati  waziri  wa  afya Zweli Mkhize  akionya  kuwa  nchi  hiyo   bado  imo   katika  njia ndefu  katika  mapambano  yake  dhidi  ya  ugonjwa  huo.

Na katika  hatari ya  maambukizi  kutokea  ndani  ya  Afrika  kusini , nchi  hiyo  imesema  maambukizi  kwa  watu  watano  kati  ya maambukizi  mapya  ni  watu  waliohudhuria  ibada  katika  kanisani linalochukua  zaidi  ya  watu 200  katika  jimbo  la  kati  la  Free State. Maafisa  wanachukua  hatua  za  haraka  kuwapata  watu wengine  waliohudhuria  ibada  hiyo.

Südafrika Kapstadt | Coronavirus | Flughafen
Abiria wakipanga msitari wakiwa tayari kusafiri kutoka Afrika kusiniPicha: Reuters/

Mfanyakazi wa hospitali aambukizwa

Kesi  nyingine  mpya  nchini  Afrika  kusini  ya  maambukizi  ni mfanyakazi  wa  hospitali  ambaye  amekuwa  katika  hospitali kadhaa  za  binafsi  nchini  humo.

Mamlaka  ya  bandari  nchini  Afrika  kusini  nayo  imesema  kwamba uchunguzi  umeonesha  kuwa  watu  waliokuwa  katika  meli  ya kitalii  pamoja  na  meli  ya  mizigo  hawana  virusi  vya  Corona , baada  ya  watu  hao  kuwekwa  katika  karantini  nje  ya  bandari  ya Cape Town kutokana  na shaka  ya  kuzuka  virusi  vya  Corona.

Hali  ya  hatari  ya  kiafya  itawekwa  nchini  Morocco  leo, wakati serikali  ikilenga  katika  kupunguza  nyendo  za  watu  ili  kuzuwia kusambaa  kwa  virusi  vya  Corona. Hatua  hizo  ambazo ni maalum, zitaanza  rasmi  usiku  wa  leo  nchini  humo, imesema wizara  ya  mambo  ya  ndani.

USA: Ausgangsperre in Kalifornien
Watu wakifanya manunuzi ya haraka kujikinga na maabukizi iwapo watazuiwa kutoka ndaniPicha: Getty Images/M. Tama

Ni  wafanyakazi  wa  sekta  maalum  tu  ndio  watakaoruhusiwa kutembea na  kwenda  makazini, kama  wafanyakazi  wa  hospitali na  mabenki  pamoja  na  wale  ambao  wanafanyakazi  katika  vituo vya  kuuzia  mafuta pamoja  na  huduma  za  chakula na  wale wanaotoa  huduma  muhimu , shirika  la  habari  la  Morocco limenukuu  duru  za  wizara  hiyo zikisema jana.

Nayo Niger  imekuwa  nchi  ya  36  barani  Afrika  kuthibitisha  kuwa na  mgonjwa  wa  COVID 19.  Mtu  huyo  anayefanyakazi  katika kampuni  ya  usafirishaji  amekuwa  mgonjwa  wa  kwanza  katika taifa  hilo  la  Afrika  magharibi .