1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ligi ya Ujerumani Bundesliga

10 Januari 2011

Bayern Munich imetoka na ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Al Wakrah mjini Doha.

https://p.dw.com/p/zvt9
Hamit Altintop wa FC Bayern Munich akiwa mjini Dubai.Picha: picture alliance/dpa

Baada ya kuwa nje kwa muda wa siku 231 kutokana na tatizo la ukano wa goti, winga mholanzi Arjen Robban alirudi japo sio kwa kishindo kwenye timu yake Bayern Munich katika mechi ya kirafiki ambayo timu hiyo ilitoka na ushindi wa mabao 4 kwa bila dhidi ya Al Wakrah mjini Doha.

Robben alionekana mwisho akiichezea timu hiyo bingwa ya Bundesliga katika fainali za ligi ya mabingwa barani Ulaya mnamo mwezi Mei iliposhindwa na mpinzani Inter Milan.

Jumamosi Robben alicheza katika awamu ya kwanza ya mechi hiyo kiashiria kwamba bado hajaimarika vilivyo kimazoezi.

Timu ya Bayern  imekuwa ikijaribu kudai kulipwa na shirikisho la soka Uholanzi  baada ya mshindi huyo wa msimu uliokwisha wa tuzo la mchezaji wa mwaka wa Bundesliga, kurudi kutoka mashindano ya Kombe la dunia Afrika kusini akiwa amechoka na kutoweza kuuanza msimu.

Sehemu ya malipo hayo itakuwa ni kuandaliwa mechi kati ya timu ya taifa ya Uholanzi na Bayern, ambayo itatia kapuni malipo ya mechi hiyo.

Robben anatarajia kuwa fiti kwa mechi ya kwanza ya Bayern baada ya mapumziko ya msimu wa baridi dhidi ya Wolfsburg siku ya Jumamosi tarehe 15.

Ama kwa upande mwingine, mchezaji wa timu ya taifa ya Ufaransa ambaye pia anaichezea timu hiyo ya Bayern, Franck Ribery, amesema ana imani kuwa timu yake itarudi katika ushindi katika awamu ya pili ya msimu wa Bundesliga na inaweza kushinda mataji mawili.

Ribery anasema pia uhusiano kati yake na kocha wa timu hiyo Louis van Gaal umemarika kwa kuwa wanaelewana sasa. Na hili linampa motisha kuwajibika zaidi kwenye timu hiyo.

Bundesliga 5. Spieltag Franck Ribery und Louis van Gaal
Frank Ribery na kocha Louis van Gaal wa Bayern Munich.Picha: AP

Bayern ipo katika nafasi ya tano kwenye orodha ya ligi hiyo ya Ujerumani baada ya mikosi mengi kwenye awamu ya kwanza ya msimu, ukiwemo kukosekana kwa Arjen Robben, na Kocha Van Gaal amesema kuifikia timu inayoongoza sasa kwenye ligi hiyo, Dortmund,  walio mbele kwa tofauti ya pointi 14, haiwezekani.

Hata hivyo Bayern bado ipo katika mashindano ya kombe la Ujerumani na mashindano ya ubingwa barani ulaya -Champions League, na itapambana na Inter katika timu 16 za mwisho ikiwa ni marudio ya mpambano wa fainali za msimu uliopita uliowapa mabingwa hao wa Italia ushindi wa mabao 2-0.

Mwandishi: Maryam Abdalla /Afpe

Mhariri: Josephat Charo