1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kombe la Ulaya

19 Juni 2008

Kesho ni zamu ya croatia na Uturuki .Holland inaisubiru Russia jumamosi..

https://p.dw.com/p/EN24

Baada ya changamoto ya kusisumua ya jana usiku kati ya mabingwa mara 3 wa Ulaya Ujerumani na Ureno, kesho jioni ni zamu ya Croatia ambayo kama Holland, ilishinda mechi zake zote 3 za duru ya kwanza.Croatia ina miadi na Uturuki mjini Vienna katika mpambano wapili wa robo-finali.

Wacroatia wanaonywa wachunge kwani waturuki walikwishuzingira mara 2 mji mkuu wa Austria, Vienna,enzi za Ottoman Empire.

►◄

Katika historia,waturuki walizimwa mara 2 kuuteka mji wa Vienna, Austria enzi za utawala wa Ottoman.Hawataki sasa kuona jaribio lao la 3 likishindwa tena leo usiku.Kuzima jaribio hilo la Waturuki,mashabiki laki 1 wa Croatia,watamiminika Vienna leo,ingawa kuna tiketi 5.400 tu zilizouzwa hadi sasa kwa mechi hii.Wenyeji Austria wameshatimuwa nje na jirani zao wajerumani.

Idadi kubwa ya mashabiki wa Croatia,wakipanga kusafiri kwa motokaa hadi Vienna ukiwa msafara wa masaa 4 tu kutoka Croatia.Wengi walipanga kuondoka usiku wa jana ili kuepuka msongamano wa magari barabarani.

Mamia ya mashabiki wa Croatia wameomba tiketi zaidi kwa mechi ya leo,lakini wameambiwa tiketi zimeadimika.Labda waturuki wamezinyakua.Kuna taarifa zisemazo bei za tiketi zimefikia hadi Euro 2000.

Croatia imezowea hadi sasa kutia mabao na mapema ,Uturuki nayo imeonesha haikati roho na mapema.Ilionesha ukaidi huo katika mapambano yake 2 yaliopita .

kama Uturuki,Russia nayo imechukua siku chache tu kugeuza mchezo wake na kuwa kikosi kikali cha kushambulia .Wamewatoa Waswede kwa mabao 2:0 hapo juzi na keshokutwa jumamosi wana miadi na Holand katika changamoto ya makocha 2 wa ki-dachi wenyewe kwa wenyewe:

Marco van Basten na Guus Hiddink.

Ikiwa kuna yeyote anaejua vipi kuvunja tumbu za lango la wadachi kesho,basi ni mdachi mwenyewe Guus Hiddink,alieiongoza Korea ya kusini hadi nusu-finali ya kombe la dunia 2002.

Kurejea kwa stadi wao wa kiungo Andrei Arshavin katika mpambano na Sweden kulibadilishi mchezo wao na kuupa nguvu.Urusi, ilitamba zaidi kuliko ilipoondoka na ushindi wa bao 1:0 dhidi ya mabingwa watetezi Ugiriki.

Kesho lakini, warusi hawtamudu kupoteza fursa nyingi za kutia mabao katika lango la Holland kama katika mpambano wao wa juzi na Sweden.

Holland,ikiegemea mastadi wao akina van Niestelrooy,van der Vaart, Van Persie na kipa Van Der Sar,haitakubali kutiwa munda na Urusi baada ya kuwachezeshakindumbwe-ndumbwei mabingwa wa dunia-Itali na makamo-bingwa Ufaransa kwa mabao 3:0 na 4:1.

Kama katika changamoto ya leo kati ya Croatia na Uturuki, mashabiki laki 1 wa Holland wanatazamiwa kuuvamia uwanja wa Eheinknie mjini Basel.

Taarifa kandoni mwa mapmbano haya 2 ya leo na kesho zasema, UEFA-shirikisho la dimba la Ulaya, linazingatia kutoa uamuzi hadi mwisho wa mwaka huu kupanua au la, idadi ya timu za finali ya Kombe hili la Ulaya.Katibu wa UEFA David Taylor alisema UEFA itawashauri wanachama wake 53 iwapo kombe la Ulaya 2016 lijumuishe timu zaidi.Ufaransa imejitolea kuandaa kombe hilo wakati Poland na Ukraine zimenyakua nafasi ya kuandaa kombe lijalo 2012 kwa ubia.

Nje ya kombe la Ulaya, Brazil jana ilitoka suluhu na mahasimu wao Argentina 0:0 katika kinyan'ganyiro cha kanda ya Amerika Kusini cha kufuzu kwa kombe lijalo la dunia 2010 nchini Afrika Kusini.