1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kocha Löw asema kambi yake siyo hospitali

26 Mei 2014

Kocha wa timu ya Ujerumani Joachim Löw amepuuzilia mbali madai kuwa kambi yake ya mazoezi nchini Italia inafanana na hospitali kutokana na idadi ya wachezaji waliojeruhiwa, akisema hali itaimarika hivi karibuni

https://p.dw.com/p/1C77P
Thomas Müller und Joachim Loew
Picha: picture-alliance/dpa

Wachezaji kadhaa akiwemo nahodha Philip Lahm, mlinda lango Manuel Neuer na kiungo Bastian Schweinshteiger wote wanaendelea kupata nafuu. Löw amesema kila mchezaji atakuwa katika hali nzuri katika siku chache zijazo.

Lahm na Neuer wanapona majeraha yao na bado hawajaanza mazoezi, wakati Schweinsteiger na beki Marcel Schmelzer akiendelea kufanya mazoezi ya kibinafsi katika kambi yao ya kaskazini mwa ITALIA.

Löw amesema wataelekea Brazil wakiwa na timu imara na yenye ushindani mkubwa. Wachezaji sasa wanafanya mazoezi yao vyema na ameridhika na namna mambo yalivyo kwa sasa.

Wakati huo huo, Sami Khedira, kiungo wa Ujerumani mwenye umri wa miaka 27 anasema ni wakati kwanza wa kusherehekea La Decima kabla ya kuweka fikra zake kwa Kombe la Dunia.

Khedira alirejea katika kikosi cha Carlo Ancelotti baada ya kuwa mkekani kwa muda mrefu kwa ajili ya jeraha alilopata mwezi Novemba mwaka jana wakati akiichezea timu ya taifa Ujerumani. Khedira alijaza pengo la Xabi Alonso katika fainali dhidi ya Atletico Madrid na akacheza kwa muda wa saa moja. Khedira alikumbuka namna Sergio Ramos alivyookoa jahazi katika fainali kwa kufunga goli katika za mwisho mwisho kabisa.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/AP
Mhariri: Yusuf Saumu