1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kinyang'anyiro cha Bundesliga chapamba moto

Bruce Amani
24 Februari 2020

Bayer Leverkusen wameimarisha matumaini yao ya kucheza kandanda la Champions League msimu ujao wakati walipopata ushindi wa 2 – 0 dhidi ya Augsburg hapo jana Jumapili.

https://p.dw.com/p/3YKJf
Fußball Bundesliga |  Schalke 04 v RB Leipzig | Torjubel (0:1)
Picha: Imago Images/Kirchner-Media/C. Neundorf

Nambari tano kwenye ligi Leverkusen sasa wana pointi sawa na Borussia Moenchengladbach, ambao wako katika nafasi ya nne na ya mwisho ya Champions League, lakini waliambulia tu sare ya 1-1 na Hoffenheim Jumamosi. Hivi ndivyo mambo yalivyokuwa katika matangazo ya moja kwa moja ya DW Kiswahili

Gladbach ambao wako mbele kwa tofauti ya mabao, wana mechi moja ya ziada, lakini pia lazima wawakabili Leverkusen Machi 22. Borussia Moenchengladbach huenda wakawekewa vikwzao baada ya mashabiki wao kuonyesha mabango kadhaa ya uchokozi uwanjani yaliyomlenga muwekezaji wa Hoffenheim Dietmar Hopp. Kocha wa Gladbach Marco Rose alilaani tabia hiyo ya mashabiki "Sisi kama shirikisho bila shaka tunaweza tu kuomba radhi kwa Hoffenheim na Bwana Hopp. Hili halistahili kuwa katika uwanja wa kandanda. Naamini pia kuwa hilo halikusaidia mhemko wa jumla uwanjani. Mashabiki wengi pia walionyesha heshima lakini napendelea kuzungumza kuhusu kandanda na sio kuhusu mambo ya aina hiyo."

Fußball Bundesliga Werder Bremen - Borussia Dortmund
Halaand anaendelea kuwasha moto katika BundesligaPicha: Reuters/F. Bimmer

Timu nyingine inayolenga kandanda la Ulaya Wolfsburg, imesonga katika nafasi ya saba baada ya kupata ushindi wa 4-0 dhidi ya nambari kumi tano Mainz.  Wolfsburg wako nyuma ya Leverkusen na Glabach na pengo la pointi tisa lakini wanawinda tikiti ya Europa League msimu ujao kama timu ya nafasi sita za kwanza itashinda Kombe la Shirikisho la Ujerumani – DFB Pokal.

RB Leipzig waliwachabanga Schalke 5 – 0 Jumamosi na kuwasogea vinara Bayern na tofauti ya pointi moja tu. Bayern walipata ushindi mgumu sana wa 3 – 2 dhidi ya washika mkia Paderborn na hata kocha Hansi Flick alikubali kuwa walisalimika "Paderbon ni wasumbufu sana na hilo pia limedhihirika leo.  Na ni muhimu sana kwamba tumecheza kandanda safi na kwa kujituma. Na tumefanya makosa madogo tu. Tulifanya makosa na kuruhusu magoli kuwa 2 - 2 na ndio maana nimeridhika na mchezo au na matokeo kwa sababu timu, lazima lisemwe, ilipambana sana hadi mwisho. Vijana walitaka kufunga bao la tatu na la ushindi na tunashukuru hilo liliwezekana."

Erling Braut Haaland aliendelea kugonga vichwa vya habari baada ya kufunga bao katika ushindi wa Borossia Dortmumd wa 2 – 0 dhidi ya Werder Bremen. Chipukuzi huyo mwenye umri wa miaka 19 alifunga bao la 12 katika mechi nane tangu alipojiunga na BVB Desemba mwaka jana. Ushindi huo umewaweka Dortmund katika nafasi ya tatu na pengo la pointi nne dhidi ya vinara Bayern.

Mechi zote za mwishoni mwa wiki zilianza kwa kuzingatia dakika moja ya kusalia kimya uwanjani kuwakumbuka wahanga wa shambulizi la itikadi kali lililotokea Hanau na kuwaua watu 9. Rais wa shirikisho la soka Ujerumani - DFB Fritz Keller alitangaza kuwa na mshikamano na wahanga wa tukio hilo "Katika kandanda, ndani na nje ya uwanja, kila kitu kinachohusu jamii jamii nzima, chuki dhidi ya wageni, ubaguzi wa rangi havina nafasi. Hii ndio njia ya kipumbavu kabisa ya kujikuta katika mambo haya, na kwa hiyo hakuna nafasi ya ubaguzi wa rangim hakuna nafasi ya chuki uwanjani."