1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kampeni za urais zaanza Misri

Admin.WagnerD30 Aprili 2012

Kampeni rasmi za uchaguzi wa rais zimeanza siku ya Jumatatu nchini Misri katika kile kinachotazamwa kama uchaguzi huru wa kwanza katika historia ya nchi hiyo.

https://p.dw.com/p/14nEf
Abdel moneim Abu al-Fatuh
Abdel moneim Abu al-FatuhPicha: picture-alliance/dpa

Wagombea kumi na watatu wanaingia uwanjani kusaka kura zitakazowesha mojawao kuwa rais wa nchi hiyo, baada ya kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja tangu kuondolewa madarakani rais wa zamani Hosni Mubarak.

Wagombea hao waliidhinishwa na Tume ya Uchaguzi ya Misri baada ya mchujo mkali uliowaacha maafisa wengi waliohudumu katika utawala wa Hosni Mubarak wakisaga meno baada ya kuengulia kutokana na kuidhinishwa kwa sheria mpya iliyotungwa na Bunge la nchi hiyo iliyowapiga marufuku wale waliohudumu katika nafasi za juu katika muongo wa mwisho wa Hosni Mubarak kugombea kiti hicho.

Amr Moussa
Amr MoussaPicha: AP

Rais wa Tume ya Uchaguzi ya Misri amewaonya wagombea hao kutothubutu kuvunja kanuni za kampeni na pia kutovuka kikomo cha matumizi wakati wa kampeni zao, lakini katika hali halisi mabango ya wogomebea hao yamekuwa mitaani kwa zaidi ya mwezi moja sasa na tayari walishaanza kufanya kampeni hata kabla ya siku rasimi siku ya Jumatatu.

Kura ya maoni yamuweka mbele Amr Moussa
Matokeo ya kura ya maoni iliyochapishwa Jumatatu na shirika la ushauri la serikali yalimuweka Katibu Mkuu wa zamani wa Jumuiya ya nchi za Kiarabu Amr Moussa mbele ya wagombea wengine kwa asilimia 41.1 ya kura. Maoni hayo yaliyoendesha na kituo cha mafunzo ya siasa na mikakati cha Al-Ahram yanaonyesha kuwa Moussa alikuwa mbele ya mwanaharakati wa kiislam mwenye msimamo wa wastani Abdul-Moneim Aboul Fatouh, ambaye alishika nafasi ya pili kwa asilimia 27.3.

Nafasi ya tatu kwa mujibu wa kura hiyo ya maoni ilienda kwa Ahmed Shafiq, kamanda wa zamani wa vikosi vya anagani na waziri mkuu wa mwisho wa Hosni Mubarak aliendolewa na kisha kurejeshwa katika kinyanganyiri hicho, akipata asilimia 11.9

Ahmed Shafiq
Ahmed SchafiqPicha: Reuters

Aboul Futouh ambaye ni kiongozi wa zamani katika chama cha Udugu wa Kiislam cha Muslim Brotherhood, amepata uungwaji mkono kutoka kwa vyama vya kihafidhina vya salafi na hivyo kuwakatisha tamaa viongozi wa udugu wa Kiislam waliotarajia vyama hivyo kumuunga mkono mgombea wake, Mohammed Mursi. Kura hii ya maoni iliendeshwa kabla wasalafi hawajatangaza kumuunga mkono Aboul Fatouh.

Kundi lingine nalo lamuunga mkono Aboul Fatouh
Chama kingine cha Gamaa Islamiya nacho kilitangaza Jumatatu kuwa kitamuunga mkono Aboul Futouh. Afisa mwandamizi wa chama hicho Assem Abdel-Maajid alisema kuwa maoni ya ndani ya chama chake yalionyesha kumuunga mkono Abdoul Futuh.

Alisema wanachama wake wameona haitakuwa vuzuri kwa chama cha Udugu wa Kiislam kuthibiti kila kitu, ikiwa ni pamoja na Bunge, urais na hata baraza la Mawaziri, hali aliyosema ni hatari kwa vuguvugu la Kiislam.

Duru ya kwanza ya uchaguzi huo inatarajiwa kufanyika kati ya tarehe 23 na 24 mwezi Mei na duru ya pili tarehe 16 na 17 Juni kama hakutakuwa na mshindi wa moja kwa moja.

Mwandishi: Iddi Ismail Ssessanga\APE\DPAE
Mhariri: Mohammed Abdul Rahman