1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jukumu jipya la Marekani kupambana na IS Iraq litaleta tija?

Zainab Aziz Mhariri: Rashid Chilumba
18 Desemba 2021

Je kwa Marekani kubadili majukumu ya majeshi yake nchini Iraq ni hatua itakayoleta mabadiliko yenye tija nchini humo?

https://p.dw.com/p/44Vt7
USA | US-Soldaten besteigen ein Flugzeug in Fayetteville, North Carolina
Picha: Capt. Robyn Haake/Planetpix/Planet Pix/ZUMA/picture alliance

Katika siku za hivi karibuni Marekani ilitangaza kwamba inayaondoa majeshi yake nchini Iraq lakini wakati huo huo ikasema inafanya mabadiliko madogo katika majukumu yake nchini humo.

Hatua hiyo ilichukuliwa miezi michache tu baada ya mkutano wa mwezi Julai kati ya Waziri Mkuu wa Iraq Mustafa al-Kadhimi na Rais wa Marekani Joe Biden. Baadaye, viongozi hao  walitangaza kwamba hakutakuwepo tena vikosi vya Marekani kwa ajili ya kuendeleza mapambano nchini Iraqi ifikapo Desemba 31, mwaka huu wa 2021.

Rais wa Marekani Joe Biden
Rais wa Marekani Joe BidenPicha: Andrew Harnik/AP Photo/picture alliance

Wachambuzi wanasema makubaliano yalifikiwa na viongozi hao wawili kwa ajili ya kupunguza shinikizo dhidi ya serikali ya Waziri Mkuu wa Iraq Mustafa al-Kadhimi. Utawala wa al-Kadhimi ulilengwa na wanamgambo wanaoungwa mkono na Iran, wanaojulikana kama Popular Mobilization Forces (PMF) nchini Iraq, ambao wanapinga uwepo wa aina yoyote wa Marekani nchini humo.

Kundi hilo na washirika wake wanashukiwa kuhusika na mashambulio yanayoendelezwa kwa kutumia ndege zisizo na rubani Pamoja na na makombora yanayolenga hususan misafara ya magari yanayobeba vifaa vya Marekani, vituo vyake pamoja na jaribio la kutaka kumuua Waziri Mkuu Mustafa al-Kadhimi mwenyewe.

Wachambuzi wamesema ndio maana mpango huo wa kubadilisha hadhi ya wanajeshi wa Marekani nchini Iraq ulikamilika kabla ya muda uliopangwa. Mnamo tarehe 9 Disemba, mshauri wa usalama wa taifa wa Iraq Qasim al-Araji alitangaza kwamba jukumu la mpito la kuishauri serikali ya Iraq, kuisaidia na kuiwezesha limekamilika.

Sasa wanajeshi wa Marekani wapo nchini Iraq kama sehemu ya operesheni ya kimataifa ambayo lengo lake ni kupambana na kundi la itikadi kali linalojiita "Dola la Kiislamu" (IS).

Waziri Mkuu wa Iraq Mustafa al-Kadhimi
Waziri Mkuu wa Iraq Mustafa al-KadhimiPicha: REUTERS

Hali ya Iraq sio kama ya Afghanistan

Licha ya hatua hizo za kubadili majukumu ya majeshi ya Marekani nchini Iraq kutangazwa kwa shamrashamra lakini mabadiliko yenyewe sio makubwa ikilinganishwa na hatua ya Marekani ya kuyaondoa majeshi yake kutoka nchini Afghanistan hivi karibuni.

Hali imebadilika kutokana na kuwa jeshi la Marekani linachukuliwa kama kikosi vamizi. Kuna hisia tofauti miongoni mwa Wairaq, baadhi yao wanataka wanajeshi hao wabakie nchini mwao huku wengime wakiwa hawataki kabisa kusikia wanajeshi wa Mareani wapo nchini mwao na wengine wanakasirishwa na kuanzishwa kwa mfululizo wa mikataba kati ya Marekani na serikali ya Iraq ambayo iliwaruhusu askari wa Marekani skuendelea kubakia nchini Iraq kwa masharti fulani.

Mabadiliko yanaendelea

Kumekuwa na mabadiliko fulani, ambayo yamekuwa yakiendelea nchini Iraq. Caroline Rose, mchambuzi mkuu katika taasisi ya wataalam ya mjini Washinton, Newlines Institute, aliiambia DW kwamba kimsingi wanajeshi wa Marekani wameziondoa kambi zao nane ambazo walidhani zinaweza kushambuliwa na kundi la PMF. Amesema hata hivyo mfululizo wa kuzihamisha kambi hizo ulifanywa kimya kimya.

Kwa mujibu wa ripoti ya mwezi Novemba kwa Bunge la Marekani kuhusu ujumbe wa jeshi la Marekani nchini Iraq, kamandi moja ilihamishwa kutoka Iraq na kuhamishiwa Kuwait mwezi mnamo mwezi huo wa Novemba na nyingine ilishushwa hadhi hivi karibuni kwa vigezo vya ukuu katika uongozi wa kijeshi.

Hadi leo hii, kuna takriban wanajeshi 2,500 wa Marekani nchini Iraq, wapo pia wakandarasi wapatao 4,500 wa Idara ya Ulinzi. Pia kuna takriban wanajeshi 1,000 kutoka nchi nyingine washirika wa Marekani waliopo Iraq na askari wapatao 130 wanatoka Ujerumani.

Mwisho wa kizungumkuti wala hauonekani

Hata baada ya kipindi cha mpito kilichotangazwa hivi majuzi, idadi ya wanajeshi wa Marekani huenda haitabadilika pakubwa, msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani John Kirby alithibitisha hilo katika mkutano na waandishi wa habari mapema mwezi huu. Kirby aliwaambia waandishi wa habari. Kwamba hay ani mabadiliko ya kawaida kulingana na makubaliano yaliyofikiwa na serikali ya Iraqi na kazi ambayo tayari ilikuwa ikiendelea kwa miezi kadhaa.

Msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani John Kirby amesema hakutakuwa na aina yoyote ya sherehe kwa ajili ya kusherehekea mabadiliko hayo na wala haitatangazwa tarehe ya mwisho ya mpango huo mpya wa mafunzo.

Msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani John Kirby
Msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani John KirbyPicha: Andrew Harnik/AP/dpa/picture alliance

Baadhi ya wachambuzi wanasema mabadiliko ya hadhi kwa wanajeshi wa Marekani nchini Iraq ni dalili ya mabadiliko yanayoendelea katika sera ya Marekani kuelekea Iraq, hasa ikilinganishwa na utawala wa rais aliyeondoka Donald Trump, mchambuzi wa Taasisi ya Brookings ya Marekani, Alaaldin amesema. "Kwa utawala huu wa sasa wa rais Joe Biden, Wairaq wanatumai Marekani itachukua mtazamo wa wastani zaidi na kuelewa kwamba hali ya usalama nchini Iraq inafungamana sana na mienendo ya kisiasa ya ndani ya nchi. Swali ni Je kubadilisha majukumu ya majeshi ya Marekani nchini Iraq ni hatua itakayoleta mabadiliko yenye tija nchini humo?

Chanzo:/https://p.dw.com/p/44U2L