1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Joachim Löw hatimaye kusitisha mkataba wake

Sylvia Mwehozi
9 Machi 2021

Kocha wa timu ya taifa ya soka ya Ujerumani Joachim Löw ataachia mikoba yake baada ya kukamilika michuano ya kombe la Ulaya, na kuondoa mipango yake ya awali ya kuondoka baada ya kombe la dunia.

https://p.dw.com/p/3qOHg
 Fußball | Nations League A | Deutschland - Ukraine
Picha: Robert Michael/dpa-Zentralbild/dpa/picture alliance

Kocha wa timu ya taifa ya soka ya Ujerumani Joachim Löw ataachia mikoba yake baada ya kukamilika  michuano ya kombe la Ulaya, na kuondoa mipango yake ya awali ya kuondoka baada ya kombe la dunia la mwaka 2022.

Shirikisho la soka la Ujerumani limesema kuwa Löw aliomba kusitisha mkataba wake ambao ulikuwa umalizike baada ya michuano ya kombe la dunia ya mwaka ujao, lakini sasa atamaliza mkataba wake mwishoni mwa mashindano ya kombe la ulaya mwaka huu.

Löw alichukua mikoba ya kuifundisha timu ya taifa ya Ujerumani baada ya kombe la dunia la mwaka 2006 na kabla ya hapo alikuwa msaidizi wa kocha Jurgen Klinsmann kwa miaka miwili.

"Ninachukua uamuzi huu kwa uangalifu, nikiwa na faraja kubwa na shukrani, lakini bado nina motisha ya kufanikiwa katika mashindano ya Ulaya", alisema kocha Löw. Löw amekiongoza kikosi cha Ujerumani kutwaa ubingwa wa kombe la dunia mwaka 2014, ukiwa ni wa nne lakini amekuwa chini ya shinikizo tangu kikosi hicho kiondolewe katika raundi ya kwanza ya michuano ya kombe la dunia iliyopita la mwaka 2018.

"Shirikisho linafahamu kile alicho nacho Jogi. Ni miongoni mwa makocha wakubwa katika ulimwengu wa soka duniani", alisema rais wa shirikisho la soka la Ujerumani Fritz Keller. "

Löw ana matumaini ya kushinda kombe la Ulaya michuano ambayo iliahirishwa mwaka uliopita kwa sababu ya janga la virusi vya corona.