1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la Syria laingia katika miji muhimu nchini humo

Amina Mjahid
7 Februari 2020

Wanajeshi wa serikali ya Syria wameingia katika mji muhimu ya kimkakati katika ngome ya mwisho ya waasi nchini humo baada ya mapigano makali na wapiganaji wa upinzani.

https://p.dw.com/p/3XP86
Syrien Aleppo Khan Tuman Soldaten
Picha: Getty Images/AFP

Mji wa Saraqeb karibu na mpaka wa Uturuki, umekuwa kitovu cha mapigano makali kwa siku kadhaa. Wapinagaji wa upinzani waliwatimua wanajeshi wa serikali ambao waliingia mjini humo Jumatano wiki hii.

Uturuki ilituma wanajeshi wapya Alhamisi na kutishia kutumia nguvu kuwalazimisha wanajeshi wa Syria kurudi nyuma ifikapo mwishoni mwa mwezi huu.

Mji huo upo katika makutano ya barabara mbili kuu, moja inayounganisha mji mkuu Damascus katika upande wa kaskazini na nyingine inayounganisha maeneo ya magharibi na mashariki ya nchi hiyo.

Shirika la habari la umma - SANA na televisheni ya inayoendeshwa na serikali Al-Ikhbariya wamesema wanajeshi wa Syria waliingia mjini humo jana usiku na wanaendelea kuwasaka waasi waliobaki pamoja na kuyategua mabomu.

Operesheni ya vikosi vya Rais Bashar al Assad kuingia katika miji na vijiji vya mkoa wa kaskazini magharibi wa Idlib imesababisha watu nusu milioni kupoteza makazi yao katika miezi miwili tu, na kuzusha janga kubwa la kibinaadamu katika jimbo hilo lililofurika watu walioachwa bila makazi.

Geir Padersen atoa wito wa kusitishwa mapigano

Syrischer Verfassungsausschuss tritt erstmals zusammen | Geir Pedersen
Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Syria Geir PadersenPicha: picture-alliance/AA/D. Aydemir

Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Syria Geir Padersen ametoa wito wa kusitishwa mara moja mapigano, kuuwekea vikwazo msaada unaotolewa kwa makundi ya kigaidi, na juhudi muhimu za kupambana na suala la wapiganaji wa kigeni

"Nnaomba kusitishwa kwa uhasama. Amani na usalama vinahitaji kwa maslahi ya kikanda na kimataifa. Na ni msingi muhimu wa mkondo wa kupatikana suluhisho la mzozo wa Syria ambao sasa unakaribia mwaka wake wa kumi," alisema Geir Padersen.

Pia mashambulizi hayo yameikasirisha Uturuki na kutishia kuzusha mzozo kati ya wanajeshi wa Uturuki na Syria. Mkuu wa masuala ya kiutu wa Umoja wa Mataifa Mark Lowcock amesema janga la kibinaadamu limeongezeka wakati mashambulizi yakiendelea kuwa makali katika maeneo ya kiraia.

Mkoa wa Idlib ni makao ya karibu watu milioni tatu, ambapo wengi wao waliyakimbia maeneo mengine ya Syria kutokana na machafuko yaliyotokea kabla.

Vyanzo: afp/ap/reuters