Javad arejea kwenye wadhifa wake baada kukataliwa kujiuzulu
27 Februari 2019Waziri wa mambo ya nje wa Iran, Mohammed Javad Zarif, alitangaza kujiuzulu ghafla kupitia mtandao wa Instagram siku ya Jumatatu jioni, siku ambayo kulikua na ugeni rasmi wa Rais wa Syria Bashar al-Assad aliyeitembelea Iran. Inasemekana kwamba Waziri huyo wa Mambo ya nje alijiuzulu kutokana na kuachwa katika mkutano huo na Rais Bashar al-Assad aliyeitembelea Iran siku hiyo na kukutana na Rais Hassan Rohani na kiongozi wa juu kabisa wa Iran Ayatollah Ali Khamenei bila kukutana na waziri huyo wa mambo ya nje Mohammen Javad Zarif.
Mtu wa karibu na Zarif aliimbia Reuters kwamba kujiuzulu kwake pia kulisababishwa na ukosoaji wa makubaliano ya mpango wa nyuklia wa nchi hiyo yaliyofikiwa pamoja na mataifa yenye nguvu duniani, lakini baadaye Marekani chini ya uongozi wa Donald Trump ilijitoa mwaka jana. Mwanadiplomasia huyo, aliyesoma nchini Marekani alikua ni kati ya watu waliofanikisha kusainiwa kwa mkataba huo ambao ulipelekea baadhi ya vikwazo dhidi ya Iran vilivyowekwa na nchi za Magharibi kufutwa.
Ofis ya Rais wa Rohani ilitoa tamko baada tu ya ujumbe huo wa waziri wa mambo ya nje kwamba rais huyo hatakubali hatua ya Zarif kujiuzulu. Mkuu wa utumisha wa Rais aliandika katika ujumbe wake wa Twitter siku ya Jumanne kwamba nchini Iran kuna sera ya mambo ya nje moja tu na waziri wa mambo ya nje mmoja tu.
Siku ya Jumatano Rouhani alikataa kujihudhuru huko kwa waziri wa Mambo ya nje akiandika kwenye barua iliyochapishwa katika shirika la habari la serikali kwamba kupokea hatua hiyo ya Zarif kutapingana na maslahi ya kitaifa ya Iran na hivyo basi anakataa kufanya hivyo.
Kufuatia hatua hiyo ya rais wa Iran, Javad Zarif alionekana Jumatano asubuhi akiwa kwenye majukumu yake ya kazi akiwa pamoja na Rais Rohani katika mahafali kwenye ofisi ya Rais mjini Tehran ya kumkaribisha Waziri Mkuu wa Armenia Nikol Pashinyan.
Mwandishi: Harrison Mwilima/DPAE/RTRE1/AFPE
Mhariri: Saum Mwasimba