1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel imepania kuendelea kuwasaka na kuwavunja nguvu waafuasi wa Hamas

27 Mei 2007
https://p.dw.com/p/CBxa

Mtu mmoja ameuwawa baada ya kombora kufyetuliwa dhidi ya mji wa Sderot nchini Israel hii leo.Tawi la kijeshi la Hamas limedai dhamana ya shambulio hilo.Waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert amesema wataendelea kuwasaka na kuwavunja nguvu wakuu wa Hamas –Ehud Olmert ameongeza kusema tunanukuu “Hakuna atakaesalimika” Mwisho wa kumnukuu waziri mkuu wa Israel.Hapo awali hujuma za madege ya kivita ya Israel ziligharimu maisha ya wapalastina watano huko Gaza.Wanajeshi wa Israel wamemkamata pia mwanachama wa pili wa Hamas,waziri wa dola Wasfi Kabaha.Alkhamisi iliyopita jeshi la Israel lilimkamata waziri wa elimu wa Palastina Nasser al Shaer na maafisa wengine wasiopungua 30 .Wapalastina kadiri 40 wameuliwa hadi sasa kufuatia siku kumi za hujuma za mabomu ya Israel huko Gaza.Israel inahoji hujuma hizo zimelengwa kuzuwia makombora ya Kassam yanayovurumishwa na wanamgambo wa Hamas dhidi ya ardhi yake.Wakati huo huo wawakilishi wa Hamas na wale wa Fatah wamekwenda Misri katika juhudi za kumaliza mvutano wa kuania madaraka kati yao.