1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran,Umoja wa Ulaya na Marekani leo zajadili juu ya mpango wa Nuklia wa Iran

Saumu Mwasimba19 Julai 2008

Ni Mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 30 Marekani kukaa meza moja na Iran

https://p.dw.com/p/Ef6C
Naibu waziri wa mambo ya nje wa Marekani William BurnsPicha: AP

Maafisa wa Iran,Umoja wa Ulaya na Marekani wanaanza mkutano wao hii leo juu ya mpango wa nuklia wa Iran huku pande zote husika zikielezea matumaini yao kwamba matokeo yatakuwa mazuri.

Mjumbe mkuu wa Iran katika mazungumzo hayo ya Nuklia Saeed Jalili atakutana na mkuu wa sera za nje wa Umoja wa Ulaya Javier Solana kuzungumzia kuhusu mpango wa vishawishi vilivyopendekezwa kwa Iran na nchi zenye nguvu.

Mazungumzo ya leo yatahudhuriwa pia na naibu waziri wa mambo ya nje wa Marekani Willliam Burns.

Marekani imebadili sera zake kuelekea Iran ambapo hapoa jana waziri wa mambo ya Nje Condoleeza Rice alikiri kwamba hatua hiyo inachukuliwa ili kuonyesha kwamba Marekani inadhamira ya kweli juu ya kuchukuliwa juhudi za kidiplomasia katika suala la Iran licha ya kwamba utawala huo wa rais Bush umekuwa mara kwa mara ukitumia matamshi makali dhidi ya Iran.

Hata hivyo amesisitiza Iran lazima ikubali kuachana na shughuli zake za urutubishaji wa madini ya Uranium kabla ya Marekani kuingia kwenye mazungumzo ya dhati na taifa hilo.

Hii ni mara ya kwanza kabisa Marekani kukaa chini na Iran tangu kuvunjika uhusiano wao miaka 30 iliyopita.