1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran yaonesha ishara ya kubadilishana meli zilizokamatwa

Sekione Kitojo
24 Julai 2019

Rais wa Iran Hassan Rouhani amedokeza ,Iran ipo wazi kwa uwezekano wa kubadilishana meli za mafuta zilizokamatwa baina ya  Uingereza na Iran na mazungumzo ambayo si ya moja kwa moja na Marekani kuhusu mpango wa nyuklia.

https://p.dw.com/p/3Mfpz
Iran | Präsident Hassan Rohani
Picha: picture-alliance/abaca/Parspix

Wakati  huo  huo kampuni inayoendesha  meli  ya  Uingereza  ya Stena Impero ambayo  ilikamatwa na  Iran siku ya  Ijumaa  imesema imefanya  mawasiliano na wafanyakazi wa  meli  hiyo. 

Supertanker Grace 1
Meli ya mafuta ya Iran iliyokamatwa nje ya eneo la GibraltarPicha: Getty Images/AFP/J. Guerrero

"Hatutaki  kuwa  na  hali  ya  wasiwasi  na  baadhi ya mataifa  ya Ulaya," Rouhani  amesema  katika  matamshi  aliyoyatoa  katika mkutano  wa  baraza  la  mawaziri yaliyowekwa  katika  tovuti  rasmi ya  serikali.

Katika  tamko  linaloashiria  wazi  kuwa  linailenga  Uingereza, Rouhani  alisema  iwapo  "wataacha  vitendo  ambavyo  si  sahihi walivyofanya, ikiwa  ni  pamoja  na  kile cha  Gibraltar, jibu  la  Iran , "litakuwa  sahihi kwa  matendo  yao.

Iran na  Uingereza  zimo  katikati  ya  mkwamo  mkubwa  kuhusiana na  maafisa  wa  Uingereza  waliokamata  meli  ya  mafuta  ya  Iran nje  ya  eneo  la  Gibraltar mapema  mwezi  Julai na  hatua  ya  Iran kukamata  meli yenye bendera  ya  Uingereza  katika  eneo  la  maji la  ghuba wiki  iliyopita.

Rouhani  pia  amesema  Iran  itakuwa  wazi  kufanya  mazungumzo iwapo  kutakuwa  na  hatua  ya  kusitisha  mapambano  katika vikwazo  vya  kiuchumi  vya  Marekani  dhidi  ya  jamhuri  hiyo  ya Kiislamu.

Uhasama  baina ya  Iran na Marekani  umeongezeka  tangu  mwaka jana  wakati  rais Donald Trump  alipoiondoa  Marekani  kutoka katika  makubaliano  ya  kinyuklia  ya  mwaka  2015 yaliyolenga kuizuwia  Iran  kuendeleza  mpango  wake wa  kinyuklia  na  kuanza kuiwekea  vikwazo.

Iran Beschlagnahmung Öltanker Stena Impero
Meli ya Stena Impero ya Uingereza iliyokamatwa na IranPicha: picture-alliance/dpa/H. Shirvani

Mazungumzo yanaendelea

"Katika  hali  hii  baadhi  ya  nchi ni wapatanishi, licha  ya  kuwa binafsi  mataifa  hayo  yanasema  wao  si  wapatanishi na  wanatoa tu  mawazo  yao," Rouhani  alisema.

Kumekuwa  na  mawasiliano  kutoka  kila  upande  katika  suala  hili na  tunaendelea  na  hilo," ameongeza.

Waziri  mkuu  wa  Japan  Shinzo  Abe alifanya  ziara  nchini  Iran mwezi  Juni  kwa  mazungumzo  yenye  lengo  la  kupunguza  hali  ya wasi  wasi  kati  ya  Iran  na  Marekani.

Mapema mwezi  huu  rais  wa  Ufaransa Emmanuel Macron alimtuma mshauri  wake  wa  ngazi  ya  juu  wa  diplomasia , Emmanuel Bonne, nchini  Iran "kuweka  pamoja  mkakati  wa  kupunguza wasi wasi".

Japan na  Ufaransa  zimekataa  kuwa  zinafanya kazi  ya  upatanishi kati  ya  Iran  na  Marekani.

Deutschland 18. Petersberger Dialog 2019 | Heiko Maas
Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani Heiko MaasPicha: picture-alliance/Flashpic/J. Krick

Waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Ujerumani Heiko Maas  yuko katika  mawasiliano  ya  karibu  na  mwenzake  wa  Ufaransa  na Uingereza , ikiwa  ni  pamoja  na  kuangalia  uwezekano  wa  ujumbe wa  pamoja  na  Ulaya  katika  eneo  la  ghuba , licha  ya  kuwa msemaji  wake  amesema  bado  ni  mapema mno  kusema  ushiriki wa  Ujerumani  utakuwaje katika  suala  hilo.

Wakati  huo  huo idara ya  ujasusi wa  ndani  nchini  Israel  imesema leo  kuwa  majeshi  ya  usalama ya  nchi  hiyo  yamefichua  juhudi za  kiintelijensia  za  Iran  kuwaandikisha  Waisrael Waarabu  na Wapalestina. Taarifa  kutoka  Shin Bet hazikutoa  idadi  ama  utaifa wa  watuhumiwa  ama  kusema  iwapo wamekamatwa  ama kufunguliwa  mashitaka  lakini  imesema  wanaoshukiwa  kuwa wafanyakazi  wa  operesheni  inayoongozwa  na  Iran wamegunduliwa katika  miezi  ya hivi  karibuni.