1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hukumu ya mauaji ya Srebrenica

27 Februari 2007

Mahkama ya kimataifa mjini The Hague ilitoa jana hukumu juu ya mauaji ya Srebrenica huko Bosnia, 1995 kutokana na kesi ya Bosnia dhidi ya serbia.Mada ya pili ni ulezi wa watoto Ujerumani.

https://p.dw.com/p/CHTc

Mada zilizo haririwa na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo ni mipango ya chama-tawala cha SPD kupanua utunzaji wa watoto wadogo kwa kuhamishia Euro bilioni 6.3 kutoka hazina ya serikali kugharimia mradi huo pamoja na hukumu iliokatwa na mahkama ya kimataifa mjini The Hague, juu ya mauaji ya waislamu kadhaa wa Bosnia huko Srevrenica.

Tukianza na gazeti la Frankfurter Rundschau kuhusu sera za familia,gazeti laandika:

“mashauri yaliotolewa na uongozi wa chama cha SPD kwa jicho la kwanza yanaonesha ni madhubuti,isipokuwa yana dosari dogo –nalo kuyapitisha kunahitaji kura za mshirika wake serikalini CDU/CSU na wahafidhina hawa wanaona hiyo ni hujuma nyengine kwa famiglia na wanapinga.

Lakini hivyo ndivyo ulivo utaratibu wa maamuzi ya kisiasa….Kwa kila hali chama cha SPD kimetoa mapendekezo yake.”

Ama gazeti la Frankfurter Allgemeine Zeitung linakosoa kwa kusema chama cha SPD kinataka kuchukua Euro bilioni 1.9 kutoka kuwapunguzia wazee wa watoto-mke na mume ili kuongeza shauku ya wanawake kufanya kazi.Wanawake kwa kutiwa mori namna hivyo watoonesha shukrani zao…..yaonesha chama cha SPD kimepanda gari moshi linalokipoteza njia.Kwani, katika nchi za Scandinevia kama Sweden,Finland na Norway ambako shule za chekechea (kindergarten) zinagharimiwa kikamilifu na kuwahudumia watoto wote kwa mingo kadhaa, hivi sasa wazee wanalipwa fedha kwa mchango wao katika jamii kwa ulezi wa watoto endapo mnamo miaka 3 ya kwanza wanasalia kulea watoto wao.”la kumbusha Frankfurter Allgemeine Zeitung.

Ama gazeti la NEUE OSNARBRÜCKER ZEITUNG lina nasaha hii:

„Chama cha SPD bora kuyazingatia tena mapendekezo yake.Ndio yana fikra nzuri ndani yake,kuachana kabisa na nyongeza za ruzuku za kuwahudumia watoto si haki.

Isitoshe ni fedha zile ziliowekwa tayari kama ruzuku kwa familia zitakazogeuzwa kugarimia nafasi za shule za chekechea.Zikitolewa fedha zaidi –hii iingekuwa ishara kwamba serikali kweli inakusudia kutekeleza jukumu lake .“

Likitugeuzia mada, gazeti la Suddeutschezeitung lajadili hukumu ya mauaji ya Srebrenica huko Bosnia, 1995 ambayo mahkama ya kimataifa mjini The Hague,jana imesema yalikua mauaji ya kuhilikisha umma.Süddeutsche Zeitung laandika:

„Mahakimu katika Mahkama hiyo mjini The Hague, wamechukua njia ya kati na kati lakini sio wamehukumu kesi iliokua mbele yao.Hukumu ya kesi ya kuhilikisha umma iliopelekwa na Bosnia dhidi ya Serbia itapalilia ugomvi hata ikiwa hukumu hiyo kwa sasa, inasaidia utulivu wa kisiasa katika Balkan.Mtu aweza kubisha sana iwapo hukumu wazi juu ya kesi hii ingelileta athari nyengine kisiasa.“

Kwa gazeti la REHEINISCHE POST linalotoka Dusseldorf, hukumu iliokatwa The Hague inampa mtu hisia za namna mbili:

Kwanza ,vigogo hasa vilivyoongoza mauaji havijatiwa nguvuni.Pili, Srebrenica lilikuwa mojawapo ya maeneo yaliolindwa na vikosi vya UM.Na hata wale waliouwawa walitegemea ahadi za kinga kutoka vikosi hivyo.

Swali linazuka:kwanini UM haukuingilia kati kuzuwia mauaji yale ? Kushindwa huko kunautwika UM jukumu la hatia kiadilifu-lasema RHEINISCHEPOST kutoka Düsseldorf.

Likituhetimishia mada hii, SAARBRÜCKER ZEITUNG laandika kwamba, kwa hukumu iliokata mahkama imepita njia inayopitika: Imetaja nani ana madhambi-jambo ambalo ni dhahiri-shahiri,inakwepa lakini kudai fidia ya kifuta machozi kwa wahanga –jambo ambalo lisingekawia kugeuka chokochoko za uhasama mpya.