1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

HRW: Marekani yamuwekea vikwazo Bensouda

Grace Kabogo
3 Septemba 2020

Shirika la kutetea haki za binaadamu lasema hatua ya utawala wa Rais Donald Trump kuweka vikwazo kwa waendesha mashtaka wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu inaonyesha kupuuzwa vibaya wahanga wa uhalifu mkubwa duniani.

https://p.dw.com/p/3hwKW
Niederlande Den Haag Internationaler Strafgerichtshof | Fatou Bensouda
Picha: Getty Images/AFP/ANP/E. Plevier

Siku ya Jumatano serikali ya Rais wa Marekani, Donald Trump ilitangaza kuweka vikwazo kwa Mwendesha Mashtaka mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, ICC Fatou Bensouda pamoja na mkuu wa idara ya sheria ya ICC na anayehusika na ushirikiano na hisani, Phakiso Mochochoko kwa kuendelea kuchunguza madai ya uhalifu wa kivita unaofanywa na Wamarekani. 

Juni 11 Rais Trump aliidhinisha vikwazo vya kiuchumi na usafiri pamoja na kutaifisha mali za watumishi wa mahakama ya ICC yenye makao yake mjini The Hague, Uholanzi, waliohusika na uchunguzi kuhusu iwapo wanajeshi wa Marekani walihusika na mateso na kufanya uhalifu wa kivita nchini Afghanistan.

Matumizi mabaya ya utawala

Mkurugenzi wa haki za kimataifa wa Human Rights Watch, Richard Dicker amesema matumizi mabaya ya utawala wa Trump kuweka vikwazo, umeundwa kwa wanaoshukiwa kuwa magaidi na wafanyabiashara wakuu wa dawa za kulevya, dhidi ya waendesha mashtaka wanaotafuta haki kwa uhalifu mkubwa wa kimataifa na inaonyesha kushindwa kwa Marekani katika kuwashtaki wahalifu wanaohusika na unyanyasaji.

Dicker anasema adhabu hiyo dhidi ya waendesha mashtaka wa uhalifu wa kivita inaonyesha kutowajali waathirika. Shirika hilo limesema amri ya rais ya mwezi Juni imeundwa sio tu kwa ajili ya kuwatisha maafisa na wafanyakazi wa mahakama hiyo wanaohusika na upelelezi muhimu, bali pia kudhoofisha ushirikiano mpana na ICC.

Bangladesch, Dhaka: Phakiso Mochochoko hält Pressekonferenz
Phakiso Mochochoko, mkuu wa idara ya sheria ya ICC Picha: Getty Images/AFP/M. Zaman

Katika kujibu amri ya rais ya mwezi Juni, nchi 67 wanachama wa ICC, wakiwemo washirika wakuu wa Marekani, walitoa taarifa ya pamoja kuelezea msimamo wao wa kuiunga mkono mahakama ya ICC kama taasisi iliyo huru na isiyoyumbishwa.

Hii iliambatana na taarifa kutoka katika Umoja wa Ulaya, watetezi wa haki za binadamu na mashirika yasiyo ya kiserikali nchini Marekani na ulimwenguni kote. Nchi wanachama za ICC zimerudia mara kadhaa kusisitiza kuiunga mkono mahakama hiyo.

''Wanachama wa ICC wameungana pamoja kabla ya kusimama na waathirika na kutetea mamlaka ya mahakama hiyo kutokana na mashambulizi yasiyo na kanuni, ikiwemo kutoka kwa Marekani,'' alisema Dicker. Amesema serikali hizo zinapaswa kuwa tayari kufanya kila linalowezekana kuhakikisha mahakama ya ICC inabaki kwenye mkondo wake, ili asitokee mtu yeyote, hata ziwe nchi zenye nguvu ambaye atakuwa juu ya sheria.

Kwa sababu ofisi ya mwendesha mashtaka ya Mahakama ya ICC inalitathmini ombi la Afghanistan na kwa sababu ya vikwazo zinavyohusiana na janga la COVID-19, mahakama hiyo kwa sasa haiendelei na uchunguzi wowote ule nchini humo.

(https://bit.ly/3hVpKdB)