1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hoffenheim imeporomolewa kileleni

10 Novemba 2008

Bayer Leverkusen imeshika usukani wa Bundesliga na Chelsea yaongoza Premier League.

https://p.dw.com/p/FqsG
Andrey Voronin (kushoto) aifumania HoffenheimPicha: AP

Hoffenheim, yatimuliwa kileleni mwa Bundesliga -Arsenal yatamba mbele ya Manchester united katika Premier League. Mkenya Paul Lekuraa aongoza wakenya wenzake kushinda Athens Marathon,nchini Ugiriki na Venus Williams atamba mbele ya Vera Zvonareva katika ubingwa wa Tennis wa WTA huko Doha.

BUNDESLIGA:

TSG Hoffenheim,wametunguliwa kutoka kileleni jana na Hertha Berlin walipochapwa bao 1:0 katika uwanja wa olimpik wa Berlin wakati mabingwa Bayern munich wameshinda changamoto yao kali na Schaslke kwa mabao 2:1 uwanjani Gelsenkirchen.

Alikuwa mtaliana Luca Toni,alierejea uwanjani baada ya kuumia muda mrefu na mfaransa Frank Ribery waliolifumania lango la Schalke na hivyo kushinda mpambano wao 5 mfululizo.Jefferson Farfan kwanza alisawazisha kwa Schalke lakini ,Ribbery akipokea pasi maridadi kutoka kwa mbrazil Ze Roberto alivunja ubishi wa Schalke uwanjani mwao.

Na hivi ndivyo alivyosema kocha wa Bayern Munich, Jurgen klinsmann baada ya ushindi huo wa kusisimua dhidi ya Schalke.

"Baada ya mechi 3 za kwanza zilizotuendea kombo dhidi ya Bremen,Hannover na halafu Bochum,tulikwishsema kuwa azma yetu ni kutawazwa mabingwa wa nusu-msimu na sasa hatutaregeza kamba kuifikia shabaha hiyo."

Kocha wa Hoffenheim,klabu ya daraja ya pili iliopanda msimu huu daraja ya kwanza na kutia fora Ralf Reinicke alisema:

" Kwa jumla,lazima kusema leo hatukucheza kama tunavyoweza kucheza.Na huwezi kuwalaumu vijana wetu kwa kuteleza leo,kwani, wiiki kadhaa sasa wamekuwa wakitamba."

Andrei Voronin alilifumania lango la Hoffenhiem mnamo dakika ya 70 ya mchezo na kuipqa Hertha Berlin ushindi ambao maana yake usukani wa Bundesliga sasa umeingia tena mikononi mwa Bayer Leverkusen ingawa nao baada ya kuongoza kwa mabao 3-0 walimalizikia sare ya mabao 3:3 na karlsruhe hapo jumamosi.

Leverkusen na Hoffenheim zote mbili zina jumla ya pointi 25 kila moja ,lakini Leverkusen yaongoza kwa magoli.mabingwa Bayern Munich wako sasa pointi 1 tu nyuma ya timu hizo 2-Leverkusen na Hoffenheim na ni shabaha yao kutawazwa mabingwa wa nusu msimu mwishoni mwa mwaka huu.Hamburg wameangukia nafasi ya 4 wakati schalke wako nafasi ya 5.Frankfurt jana ilimudu sare tu mabao 2-2 na Stuttgart.

Msangao ulizushwa pia na timu nyengine iliopanda msimu huu daraja ya kwanza kutoka ya pili pamoja na Hoffenheim:FC Cologne.Cologne ilitamba nyumbani hapo ijumaa jioni ilipotoka nyuma na kuitoa Hannover kwa m abao 2:1.

Katika Premier League-Ligi ya Uingereza,Chelsea iliadhimisha siku ya kuzaliwa kwa kocha wake mbrazil Felipe Scolari ya kutimu mwaka wa 60 jana kwa kuparamia tena kileleni mwa Premier League.Chelsea iliikomea Blackburn Rovers mabao 2:0.Sasa Chelsea iko sare kwa pointi na Liverpool,lakini inaongoza kwa magoli.Ilikuwa mfaransa Nicolas Anelka alietia mabao yote 2 .Liverpool iliizaba West Bromwich mabao 3-0.Siku moja kabla hapo jumamosi, Arsenal ilitamba mbele ya Manchester United ilipoikomea Manu mabao 2-1.

Katika serie A, ligi ya Itali, mabingwa Inter Milan wamenyakua jana usukani wa Ligi hiyo kufuatia ushindi wa bao 1:0 dhidi ya Udinese.Alikua julio Cruz alielifumania lango la Udinese.Napoli sasa wana pointiu 23 ,pointi moja nyuma ya viongozi Inter Milan.Napoli waliichapa Sampdoria mabao 2:0 .Jumamosi Roma ilimudu suluhu tu ya bao 1:1 na Bolognia wakati Torino iliizaba Palermo bao 1:0.

Ushindi wa mabao 2-1 jana wa Villarreal dhidi ya Almeria, umejongeza villareal nafasi ya pili katika la Liga-Ligi ya Spain. Villareal yuko pointi 1 mbele ya Real Madrid ilioangukia nafasi ya tatu na ilioitandika Malaga mabao 4-3.

Katika medani ya riadha,mkenya Paul Lekuraa aliwaongoza wakenya wenzake kutamba katika Athens-marathon nchini ugiriki hapo jana.Huo ukawa ushindi 5 mfululizo kwa Kenya.

Lekuraa alimpiku Julius Kiprotich kuchukua ushindi huku wote 2 lakini wakichukua muda wa masaa 2: 12 na sek.42.Paul kogo akatokea 3 kwa muda wake wa masaa 2:12:49.

Zadi ya wanariadha 4,600 walishiriki katika mbio hizi za marathon mjini Athens.

Katika medani ya Tennis ,Venus Williams wa Marekani, alimshinda jana Vera Zvonareva huko Doha,Uarabuni kwa seti 3-6-7-6-0 na 6-2 ili kutwaa ubingwa wa WTA kwa mara ya kwanza na miaka 7 tangu dada yake Serena kutwaataji hilo.