1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hezbollah washindwa katika uchaguzi Lebanon.

8 Juni 2009

Hezbollah wameshindwa katika uchaguzi muhimu kabisa nchini Lebanon.

https://p.dw.com/p/I5S2
Saad Hariri, Muungano wake unaoungwa mkono na nchi za Magharibi washinda Lebanon.Picha: AP

Muungano unaoungwa mkono na nchi za Magharibi umeshinda katika uchaguzi mkuu nchini Lebanon. Mseto huo wa vyama unaongozwa na Saad Hariri, mwanawe, waziri mkuu aliyeuawa Rafiq Hariri uliiushinda muungano wa upinzani wa kundi la Hebollah, katika uchaguzi uliokuwa unaangaliwa kwa makini na jumuiya ya kimataifa.

Libanon Siegesfeier der Hisbollah in Beirut Scheich Hassan Nasrallah
Kiongozi wa Hezbollah, Sheikh Hassan Nasrallah. Muungano wao washindwa Lebanon.Picha: AP

'' Wamevunjika.........na Lebanon imeibuka mshindi''- Ndio ilikuwa kichwa cha gazeti moja nchini Lebanon baada ya kuibuka kuwa Muungano wa Saad Hariri unaopinga ushawishi wa Syria nchini Lebanon umeshinda katika uchaguzi wa jana. Uchaguzi nchi za Magharibi ulikuwa unauangalia kwa makini- baada ya kubashiriwa kuwa kundi la Hezbollah wanaoungwa mkono na Syria na Iran heunda wakashinda.


Gazeti la Al- Mustaqbal linalomilikiwa na Saad Hariri lilisema muungano wake unaojulikana kama '' March 14'' umeshinda viti 71 vya ubunge- ukilinganisha na 57 vya Hezbollah katika bunge hilo la viti 128.


Na ingawa matokeo rasmi hayajatangazwa - hili halikumzuia Hariri kusherehekea ushindi na wafuasi wake- akisema hii ilikuwa siku kubwa nchini Lebanon.

'' Nawapongeza nyote , uchaguzi huu hauna mshindi na aliyeshindwa ...mshindi pekee ni demokrasia na mshindi mkubwa ni Lebanon.'' Alisema Hariri.


Kundi la Hezbollah pia lilisalimu amri na kuridhia limeshindwa kudhibiti bunge la Lebanon. Mwanasiasa mmoja mfuasi wa kundi hilo alinukuliwa akisema matokeo ya uchaguzi huu yanaonyesha raia nchini Lebanon walitishwa wasiwapigie kura Hezbollah kwa kisingizio kuwa kundi hilo litaamrisha kuwepo kwa sheria ya dini ya Kiislamu nchini humo.


Wachanganuzi wa kisiasa sasa wanatafakari uwezekano wa mahasimu hawa wawili wa kisiasa nchini Lebanon- kuunda serikali ya umoja wa kitaifa kuhakikisha Lebanon haitumbukii katika dimbwi la machafuko mapya na vita vya kimbari.


Symbolbild Beziehungen Syrien Libanon Assad und Nasrallah
Hezbollah wanaungwa mkono na Syria.Picha: AP

Polisi na wanajeshi wametawanya katika sehemu inyokisiwa huenda kukazuka mapigano- lakini hadi kufikia sasa Lebanon ni tulivu. Wakati huo huo, waziri mmoja nchini Israel ametolea mwito muungano ulioshinda uchaguzi kuchukua hatua ya kwanza ya kuwanyanganya silaha kundi la Hezbollah. Ushawishi wa Hezbollah, Lebabon hasa unatokana na kwamba wana jeshi lenye nguvu zaidi nchini humo.


Matokeo rasmi ya uchaguzi yatajulikana baadaye hii leo. Aslia mia 54 ya watu walijitokeza kupiga kura katika uchaguzi huu uliosemekana ndio muhimu kabisa katika historia ya Lebanon- tangu kumalizika kwa vile vita vya wenyewe kwa wenyewe vya mwaka wa 75 hadi 91.

Aliyekuwa rais wa Marekani Jimmy Carter aliyeongoza kundi la wachunguzi wa kimataifa katika uchaguzi huo alisema ana matumaini, vyama vya kisiasa nchini Lebanon na Washirika wao katika nchi za nje watakubali matokeo ya uchaguzi.

Makundi ya wachunguzi wa Lebanon na wenzao wa jumuiya ya kimataifa wamesema uchaguzi huo ulikuwa huru licha ya matatizo kadhaa ya taratibu za uchaguzi.


Mwandishi: Munira Muhammad/ AFPE

Mhariri:M.Abdul-Rahman