Hali yazidi kuvurugika nchini Syria
10 Januari 2012Kutokana na hali inayozidi kuwa mbaya na shinikizo linalozidi kukuwa, rais Bashar al Assad amehutubia taifa kwa njia ya televisheni punde hivi na kuyalaumu makundi ya kigeni na vyombo vya habari vya kigeni kujaribu kuvuruga hali ya mambo nchini mwake.
"Makundi ya kimkoa na kimataifa yanayojaribu kuvuruga hali ya mambo nchini Syria hayawezi kughushi matukio" amesema rais Bashar al Assad anaehoji yeye ndie aliyeitolea mwito jumuia ya nchi za kiarabu iingilie kati.
Rais Bashar al Assad ameonya dhidi ya miito ya kuisitishia nchi yake uwanachama wa umoja wa nchi za kiarabu na kusema wanaweza kufanya hivyo, lakini haimaanishi wataipokonya Syria asili yake ya kiarabu.Rais Bashar al Assad amesema milango ya nchi yake iwazi kwa umoja wa nchi za kiarabu kusaka ufumbuzi wa mzozo wa nchi hiyo kwa sharti lakini wanaheshimu "mamlaka ya Syria."
Tume ya uchunguzi ya umoja wa nchi za kiarabu imewasilisha ripoti yake kuhusu hali namna ilivvyo nchini Syria. Hata hivyo, upande wa upinzani wa Syria unaikosoa ripoti hiyo na kusema haiambatani na ukweli wa mambo.
Wanataka kadhia ya Syria ikabidhiwe baraza la usalama na patengwe maeneo marufuku k wa safari za ndege ili kuwahifadhi raia.
Uturuki inayomshinikiza rais Assad ang'atuke imeonya dhidi ya hatari ya kuzuka vita vya wenyewe kwa wenyewe na vita vya kidini nchini Syria.
Kiongozi wa kanisa katoliki ulimwenguni Benedikt wa 16 ametoa mwito kwa upande wake wa kuendelezwa "mdahalo wa maana" na kusimamiwa na wachunguzi huru ili kama alivyosema,kukomesha umwagaji damu nchini humo.
Wakati huo huo, mufti mkuu wa Syria Sheikh Ahmad Badreddine Hasoune akihutubia katika ibada ya pamoja kati ya waislam na wakristo kuwakumbuka wahanga 26 wa shambulio la ijumaa iliyopita mjini Damascus amewatolea mwito wapinzani "waweke chini silaha."
Askofu mkuu Luka al Khouri aliyeongoza ibada hiyo amekosoa kwa upande wake "vikwazo vinavyoathiri uchumi wa nchi hiyo.
"Wanaowawekeya vikwazo wasyria na kuhatarisha mkate wao,hawamjui,si Kristo,si tafsiri ya demokrasia,haki za binaadam na wala utu."
Kwa upande mwengine, waziri wa habari Adnane Mahmoud amesema vyombo 136 vya habari vya kutoka nchi za kiarabu na vya kigeni vimepatiwa kibali cha kuingia na kufanya kazi ili kuripoti kuhusu hali ya mambo nchini Syria.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP/Reuters
Mhariri: Miraji Othman