1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ghana yaingia robo fainali kombe la dunia

27 Juni 2010

Ushindi wa Ghana hapo jana dhidi ya Marekani, umewafanya wawakilishi hao pekee wa Afrika waliyobakia katika kombe la dunia, kuwa nchi ya tatu kufikia hatua ya robofainali na kufuata nyayo za Cameroon na Senegal.

https://p.dw.com/p/O4KN
Asamoah Gyan akiifungia Ghana bao la ushindi dhidi ya MarekaniPicha: AP

Ushindi huo ulipokewa kwa sherehe na furaha kubwa kote barani Afrika, na kuchukuliwa kama ushindi wa Afrika.Katibu Mkuu wa Chama cha soka cha Rwanda Jile Karisa amesema Ghana imeonesha mfano wa kuigwa na nchi nyingine za kiafrika

Vyombo vya habari nchini Afrika Kusini, viliunadi ushindi huo wa Ghana vikisema, Ghana yazima ndoto za Marekani.Chama kinachotawala nchini Afrika Kusini cha ANC kilitoa taarifa rasmi kuipongeza Ghana.

Katika fainali zilizopita Ghana iliifunga Marekani.Marekani katrika mechi ya jana ilikuwa na hamu ya kulipiza kisasi, lakini Asomah Gyan alizima ndoto hizo pale alipopachika bao la pili pale mpambano uliporefushwa muda na kwa furaha alisema.

´´Mimi ni binaadamu mwenye furaha sana duniani.tuliwafunga katika fainali zilizopita na tumewafunga tena, lakini safari hii tumesonga mbele zaidi, kwakweli nina furaha sana´´

Fußball WM 2010 Südafrika Achtelfinale USA Ghana
Wachezaji wa Ghana wakishangilia bao la kwanzaPicha: AP

Ghana sasa itapambana na Uruguay katika robofainali hapo siku ya Ijumaa.Uruguay ilifanikiwa kufuzu kwa hatua hiyo baada ya hapo jana nayo pia kupata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Korea Kusini.

Hii leo macho na masikio ya washabiki wa kabumbu kote duniani yanaelekezwa katika pambano la mahasimu wa jadi wa soka Ujerumani na Uingereza.Hapa Ujerumani kwa takriban siku tano habari zilizohanikiza katika vyombo vya habari ni juu ya pambano hilo.

Wachezaji wa timu ya taifa ya Ujerumani wameahidiwa donge nono iwapo wataibwaga Uingereza.Shirikisho la soka la Ujerumani DFB limewaahidi wachezaji hao kitita cha Euro 50,000 iwapo wataibuka na ushindi na nyongeza ya euro 100,000 iwapo wataingia nusufainali, Euro 150,000 kwa fainali na Euro 250,000 kwa kutwaa ubingwa.

Mwandishi:Aboubakary Liongo

Mhariri:Mohamed Dahman