1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Gaidi mtuhumiwa Salel Ali Saleh Nabhan auliwa Somalia

Oumilkher Hamidou15 Septemba 2009

Opereshini za helikopta za Marekani zimepelekea kuliwa gaidi aliyekua akisakwa na FBI

https://p.dw.com/p/Jgri
Mwanaharakati wa Al Shabab mjini MogadischuPicha: AP

Saleh Ali Saleh Nabhan,mkenya anaetuhumiwa kushiriki katika mashambulio ya kigaidi ya Al Qaida mjini Mombasa mnamo mwaka 2002,ameuliwa kufuatia hujuma za vikosi vya Marekani kusini mwa Somalia.

Opereshini zilizofanywa jana na helikopta za kijeshi za Marekani,zililengwa kijiji cha kusini cha Somalia-Erile karibu na mji wa Barawa eneo linalodhibitiwa na wanamgambo wa kiislam wa Shabab,wanaojitambulisha moja kwa moja na mtandao wa kigaidi wa Al-Qaida na kiongozi wake Ossama Ben Laden.

Kwa mujibu wa mashahidi opereshini hizo za helikopta nne za kimarekani zililenga gari iliyokua imesheheni abiria .Baada ya shambulio hilo,baadhi ya abiria hao walipandishwa ndani ya helikopta hizo.

Kwa mujibu wa vituo vya televisheni vya Marekani-ABC na Fox,angalao helikopta moja ilifyetua risasi dhidi ya gari hilo lililokua likiwasafirisha wafuasi wa Al Qaida.Kwa mujibu wa afisa mmoja aliyenukuliwa na kituo cha televisheni cha ABC,manuari ya vikosi vya Marekani haikua mbali na mahala opereshini hiyo lilikotokea,tayari kuingilia kati pindi ingehitajika.

Inaaminiwa kwamba Al Shabab wanasaidiwa na wakuu kadhaa wa al Qaida,ikiwa ni pamoja na Saleh Ali Saleh Nabhan.

Mtuhumiwa huyo wa kigaidi alikua katika orodha ya watu wanaosakwa kwa udi na ambari na idara ya polisi ya shirikisho ya Marekani-FBI,akihusishwa na shambulio dhidi ya hoteli moja inayomilikiwa na waisrael,lililogharimu maisha ya watu 15,November 28 mwaka 2002-mjini Mombasa Kenya.

Sambamba na shambulio hilo makombora mawili yaliyovurumishwa na magaidi yaliikosa shabaha ya kuidengua ndege ya Israel mara baada ya kuruka kutoka uwanja wa ndege wa mji huo.Mtandao wa al Qaida ulidai kuhusika na mashambulio hayo.

Wafuasi wa itikadi kali ya dini ya kiislam Al Shabab wametishia kulipiza kisasi kwa kuuliwa Saleh Ali Saleh Nabhan.

Kwa upande mwengine kundi hasimu la Ahlu Sunna limeshangiria kuingilia kati vikosi vya kimarekani na kumuuwa mmojawapo wa wanaharakati wa Al Shabab.

Ahlu Sunna wanashauri opereshini zaidi kama hizo zifanyike ili kama wanavyosema "kuitakasa Somalia na wanamgambo wa kigeni wa kiislam".

Karte von Somalia
Ramani ya Somalia nchi ya pembe ya Afrika inayopakana na bahari ya Hindi na ujia wa maji wa AdenPicha: AP

Serikali ya mjini Washington inahofia Somalia inayosumbuliwa na ugonvi kati ya serikali na makundi ya waasi wa kiislam isije ikageuka ngome ya wafuasi wa itikadi kali kama yalivyo maeneo ya mpakani ya Afghanistan na Pakistan.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP/Reuters

Mhariri:M.Abdul-Rahman