1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Eduardo dos Santos: Rais wa milele wa Angola afariki dunia

8 Julai 2022

Kwa miongo kadhaa aliiongoza Angola kwa mkono wa chuma.Baadhi walimsifu na wengine wakamkosoa. Hivi sasa Jose Eduardo dos Santos amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 79.

https://p.dw.com/p/4DsRO
Jose Eduardo dos Santos
Picha: Paulo Novais/EPA/dpa/picture alliance

Jose Eduardo dos Santos alikuwa mmoja wa nchi waliohudumu kwa muda mrefu zaidi barani Afrika na alichangia historia ya nchi yake kwa miongo kadhaa. Wakati anazaliwa Agosti 28, 1942, Angola ilikuwa bado koloni la Ureno.

Akiwa na umri wa miaka 16, alijiunga na vuguvugu la ukombozi la MPLA, lililopigania uhuru wa Angola. Baada ya vuguguvu hilo kuanzisha mapambano ya uhuru ya silaha mnamo 1961, dos Santos alikimbilia uhamishoni. Baadae alisomea katika iliyokuwa Jamhuri ya Kisovieti na kuhitimu kama mhandisi wa petroli. Mwaka 1970 alirejea nchini mwake.

Soma pia: Rais wa zamani wa Angola José Eduardo Santos afariki dunia

Baada ya uhuru mwaka 1975, dos Santos aliteuliwa kuwa waziri wa mambo ya nje, huku MPLA ikijibadili na kuwa chama cha siasa. Dos Santos na makomredi wenzake waliunda utawala wa chama kimoja chenye msingi wake kwenye ruwaza ya kisovieti.

Muda si mrefu vikazuka vita vya wenye kwa wenyewe na vuguvugu la UNITA, lililokuwa linaungwa mkono na Afrika Kusini na Marekani. Dos Santos alikuwa anajijenga kisiasa akiwa waziri wa mipango na naibu waziri mkuu. Mnamo 1979 alifanikisha lengo lake: baada ya kifo cha Agostinho Neto, alichukuwa urais na uongozi wa MPLA.

Amani kama mradi mkubwa wa kisiasa

Jose Eduardo dos Santos
Jose Eduardo dso Santos enzi za uhai wake.Picha: Themba Hadebe/AP/picture alliance

Wakati huo vita vya wenyewe kwa wenyewe viliendelea na ilikuwa baada tu ya kuuawa kwa kiongozi wa waasi Jonas Savimbi katika mapigano mwaka 2002, ndipo nchi hiyo ilipata utulivu. Dos Santos pia ilifanya upatanishi katika mizozo nchini Jahmhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Soma pia:Rais wa Angola hataki mazungumzo na dos Santos 
Wakosoaji hata hivyo wana mtazamo tofauti, kwa sababu Santos pia aling'angania madarakani. Mwaka 2001 alitangaza kwa mara ya kwanza kwamba hangewania tena katika chaguzi zinazofuata. Hata hivyo alirejea miaka saba baadae. Mwaka 2010 bunge lilipitisha katiba mpya ambapo kiongozi wa chama chenye nguvu zaidi alipita moja kwa moja kuwa rais.

Katika uchaguzi wa bunge wa mwaka 2012, chama tawala cha MPLA kilirejesha wingi wake, na Dos Santos alisalia kuwa rais. Waangalizi wa uchaguzi walisema upinzani haukupata haki katika uchaguzi.

Haikuwa hadi 2017 ambapo dos Santos aliamua kutogombea tena. Joao Lourenco aliapishwa kuwa mrithi wake Septemba 26, 2017. Hata hivyo dos Santos aliendelea kuongoza chama hata baada ya kujiuzulu.

Kwa kutumia pesa na madaraka, aliendelea kulidhibiti bunge, mahakama na serikali huku vyombo vya habari na upinzani vikitishiwa. Upinzani ulimkosoa kwa upendeleo uliokithiri. Dos Santos pia alikuwa na ushawishi mkubwa kwenye sera ya kiuchumi.

Angola tajiri, Waangola maskini

Alihama rasmi kutoka nadharia za Kimarxi katika miaka 1990 na kuanzisha uchumi wa kimasoko. Matokeo yake ni Angola kukuwa na kuwa na uchumi wa tatu mkubwa barani Afrika na ya pili kwa uzalishaji mafuta.

Mnamo mwaka 2014, Jarida la Afrika lilimtaja dos Santos kuwa mtu wa mwaka kutokana na mchango wake kwenye maendeleo ya kiuchumi ya Angola.

Angola Präsident Joao Lourenco
Rais wa sasa wa Angola Joao Lourenco.Picha: imago images/NurPhoto

Licha ya utajiri mkubwa wa mafuta hata hivyo, watu wengi nchini Angola hawanufaiki na rasilimali hiyo. Zaidi ya nusu ya wangola wanaishi chini ya kiwango cha umaskini, huku ukosefu wa ajira ukiwa mkubwa na asilimia 87 ya wakaazi wa mjini wakiishi kwenye maeneo ya mabanda.

Baadhi wanasema maisha yalikuwa mazuri zaidi chini ya utawala wa kikoloni wa Ureno kuliko ilivyokuwa chini ya Dos Santos.

Nchi yageuka kuwa biashara ya familia

Wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe, Eduardo dos Santos alichukuwa kampuni kadhaa za kujimilisha mwenyewe. Baadae bunge la Angola lilimpiga marufuku rais huyo kumiliki hisa katika kampuni za kibiashara.

Serikali ya Angola inavyokabiliana na muziki wenye ukosoaji

Soma pia:Binti wa rais wa zamani wa Angola anakanusha madai ya ufisadi 

Kufuatia marufuku hiyo, aliamua kutoa hisia za makampuni hayo kwa binti yake Isabel dos Santos, ambaye alitajwa na jarida la Forbes kuwa mwanamke tajiri zaidi barani Afrika.

Lakini hali hiyo ilibadilika chini ya utawala wa sasa wa Joao Lourenco, alieonyesha dhamira ya kweli ya kupambana na rushwa na na uungumtu. Kama mmoja ya hatua zake za kwanza akiwa rais, alimfuta kazi Isabel dos Santos kutoka kampuni ya taifa ya mafuta.

Kaka yake Jose Filomeno dos Santos alihukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani mwaka 2020 baada ya kesi iliyodumu kwa muda mrefu, na alitimuliwa mara moja na rais Lourenco kama mkuu wa wakfu wa taifa wa maduta wenye thamani ya dola bilioni 5.