1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Droo ya awamu ya mchujo ya Champions League

16 Desemba 2013

Mabingwa watetezi Bayern Munich watacheza na Arsenal wakati nao mabingwa mara nne Barcelona wakipambana na Manchester City katika awamu ya mchujo ya Ligi ya Mabingwa Ulaya - UEFA Champions League

https://p.dw.com/p/1AaRg
Champions League Auslosung 16. Dez. 2013
Picha: FABRICE COFFRINI/AFP/Getty Images

Droo ya awamu ya timu 16 bora ya UEFA Champions League, imefanywa leo katika makao makuu ya shirikisho la Soka Ulaya, mjini Nyon Uswisi. Mabingwa mara tisa wa Ulaya Real Madrid watashuka dimbani na timu ya Bundesliga Schalke 04, wakati makamu bingwa wa msimu uliopita Borussia Dortmund wakikutana na Zenit St Petersburg wa Urusi.

Mabingwa mara tatu Manchester United wa Uingereza watakabana koo na mabingwa wa Ugiriki Olympiakos, huku mabingwa mara saba AC Milan wa Italia wakicheza na Atletico Madrid wa Uhispania. Bayer Leverkusen wa Ujerumani wakutana na miamba wa Ufaransa Paris St Germain, nao Cheslea wa Uingereza wakimkaribisha tena Didier Drogba na kikosi chake cha Galatasaray.

Mechi za mkondo wa kwanza zitachezwa Februari 18 na 19, na 25 na 26. mikondo ya pili itakuwa Machi 11 na 12, na 18 na 19. fainali itakuwa mjini Lisbon mnamo Mei 24, katika uwanja wa Estadio da Luz

Mwandishi: Bruce Amani/DPA/AFP

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman