1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dakika Moja ya kuomboleza vifo vya watu 93 nchini Norway

Abdu Said Mtullya25 Julai 2011

Watu 93 waliouawa katika mashambulio mawili ya kigaidi wakumbukwa nchini Norway

https://p.dw.com/p/122jo

Watu nchini Norway leo adhuhuri watanyamaza kimya kwa muda wa dakika moja ili kuombeleza vifo vya wananchi wenzao 93 waliouawa kutokana na mashambulio mawili ya kigaidi ijumaa iliyopita.

Polisi ya nchi hiyo imesema mtu alieyafanya mashambulio hayo amekiri kwamba yalikuwa ya kikatili, lakini amesema yalikuwa ya lazima. Mtuhumiwa huyo mwenye umri wa miaka 32 anatazamiwa kufikishwa mahakamani leo.

Hapo jana sala ya kuomboleza vifo vya watu hao ilifanyika kwenye kanisa la Oslo. Mfalme Harald wa Norway pamoja na Waziri Mkuu Jens Stoltenberg pia walihudhuria.

Watu walioshuhudia mashambulio hayo wamesema mtu aliejifanya kuwa polisi alifyatua risasi kwenye kisiwa cha mapumziko kilichopo kaskazini magharibi ya mji Mkuu Oslo. Idadi kubwa ya waliouawa walikuwa vijana waliokuwa kwenye kambi hiyo ya chama cha Labour kinachotawala nchini Norway.

Hapo awali watu saba pia waliangamizwa kutokana na mlipuko karibu na makaazi ya serikali mjini Oslo Ijumaa iliyopita.Polisi wamesema mlipuko huo ulitokana na bomu lililotegwa ndani ya gari na mshambuliaji huyo huyo.