1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chama Kipya SADC chaundwa nchini Africa Kusini.

Ponda, Eric Kalume3 Novemba 2008

Nchini Africa Kusini kundi lililojitenga kutoka kwa chama cha African Nationa Congresss ANC; hatimaye limesajili chama kipya South African Democratic Congress SADC kupambana na ANC ya Jacob Zuma.

https://p.dw.com/p/FmYA
Rais wa ANC nchini Africa Kusini, Jacob Zuma anayekabiliwa na upinzani ndani ya chama chake.Picha: AP


Hata hivyo hatua imepuuzwa na kundi la Jacob Zuma likiwataja wanachama hao kuwa nyoka wenye sumu.



Kuundwa kwa chama hicho cha SADC, kunafuatia malumbano makali ambayo yamekuwa yakiendelea kwa muda sasa tangu kujiuzulu kwa aliyekuwa rais wa nchi hiyo Thabo Mbeki, kutokana na tofauti za kisiasa baina yake na rais wa chama chsa ANC Jacob Zuma.


Akitangaza kuundwa kwa chama hicho cha SADC, kiongozi wa muda wa chama hicho Mbhazima Shilowa alisema, wako tayari kuchukua uongozi wakati uchaguzi mkuu utakapoitishwa mwakani.


Kusajiliwa kwa chama hicho, hatimaye kumebadili siasa nchini Africa Kusini, siasa ambazo zimedhibitiwa na chama cha ANC tangu taifa hilo kujipatia uhuru wake mwaka wa 1994.


Viongozi wa chama hicho wanasema kuwa sherehe rasmi ya kuanzisha kampeini za chama hicho kipya kuchukua uongozi wakati wa uchaguzi mkuu ujao mwakani, zitafanyika tarehe 16 mwezi Disemba, hatua ambayo imepuzwa na Jacob Zuma, akisema kuwa kamwe ANC hakitatingishwa na watu hao aliowataja wasaliti na kuwafananisha na nyoka wenye sumu.


Hatua ya kuundwa kwa chama hicho cha SADC imezua hisia mbali mbali miongoni mwa wafuasi wa chama hicho, huku wengine wakiitaja kuwa ifaayo katika kukuza demokrasia nchini Africa Kusini.


"Sidhani kuundwa kwa chama hiki kipya ni kupinga ANC, la hasha, lengo hasa ni kurekebisha makosa ndani ya chama hicho cha ANC na naamini lazima tuwe na chama kingine cha upinzani ili kuwa fursa raia wa Africa kusini nafasi hiyo. Bado tunasafari ndefu". alisema raia mmoja nchini humo Loco Makalema.




Kwa upande wake kiongozi wa muda wa chama hicho Mbhazima Shilowa alisemsa kuwa chama hicho hakipanii kuwa katika upande wa upinzani bali kushinda uchaguzi na kuunda serikali ijayo.


Mgawanyiko ndani ya chama cha ANC ulianza kujitokeza mwezi Disemba mwaka uliopita wakati Jacob Zuma alipomshinda Thabo Mbeki kama rais wa Chama cha ANC, na kisha tofauti hizo kumalizikia mahakamani pale Jacob Zuma alipokabiliwa na mashtaka ya Ufisadi na kutumia vibaya mamlaka.


Hata hivyo mahakama ilimuondolea mbali mashtaka yaliyomkabili Jacob Zuma, huku kukiwa na tetesi kwamba kesi hiyo ilikuwa imechochewa kisiasa.


Hii ilipelekea kujiuzulu kwa Thabo Mbeki pamoja na baadhi ya mawaziri waliokuwa wakihudumu katika serikali yake mwezi Septemba, hali iliyopeleka mpasuko huo zaidi ndani ya ANC.

Licha ya kuundwa kwa chama hicho Thabo Mbeki hajajitokeza hadharani kuunga mkono chama hicho kipya, ingawa wiki iliyopita alimuandikia rais wa chama cha ANC Jacob Zuma kumuelezea kuwa hatashiriki katika kumpeini za chama cha ANC hapo mwakani.


Jacob Zuma anaungwa mkono na zaidi ya asilimia 43 ya raia nchini Africa Kusini pamoja na muungano wa vyama vya wafanyi kazi nchini humo.