1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bush na Putin wakutana kujaribu kutatua mvutano

6 Aprili 2008

-

https://p.dw.com/p/Dco2

SOCHI

Rais George W Bush wa Marekani na mwenzake wa Urussi Vladmir Putin wataanza rasmi hii leo mazungumzo yao ya ana kwa ana ya kujaribu kuutengeneza uhusiano baina ya nchi hizo mbili lakini hakuna matumaini ya kuuyatatua masuala muhimu ya mpango wa Marekani wa kutaka kuweka mifumo ya makombora ya ulinzi barani Ulaya ambayo yanasababisha mvutano uliopo.Urussi inapinga vikali mpango huo wa Marekani ambao unataka kuwekwa kwa mtambo wa kuzuia makombora nchini Poland na mtambo wa Radar katika Jamhuri ya Czech.Viongozi hao wawili walianza mkutano wao wa kuagana hapo jana katika eneo hilo la Sochi ambapo walikula chakula cha jioni na kutumbuizwa na ngoma za kitamaduni za urussi.Wanatazamiwa kutiliana saini mpango wa mikakati juu ya uhusiano wa baadaye baina ya mataifa hayo mawili.

Mkutano huu unakuja baada ya mkutano wa kilele wa jumuiya ya kujihami ya nchi za magharibi NATO uliofanyika Romania ambapo rais Putin ambaye alikuwa mgeni katika kikao hicho alionya dhidi ya kujipanua kwa muungano huo.Mkutano wa Nato pia ulikubaliana kuiunga mkono Marekani katika mpango wake wa makombora ya ulinzi.Rais Bush pia amepangiwa kukutana na rais mteule wa Urussi Dmitry Medvedev.