1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bundesliga na ubingwa wa riadha Osaka,japan:

Ramadhan Ali31 Agosti 2007

Mwishoni mwa wiki macho yanakodolewa mashindano ya ubingwa wa riadha nchini Japan,kombe la klabu bingwa barani Afrika na Bundeslia.

https://p.dw.com/p/CHb6
Bundesliga uwanjani leo
Bundesliga uwanjani leoPicha: AP

Bayern Munich ambayo msimu huu imekosa tiketi ya champions League-kombe la klabu bingwa barani Ulaya, imeanza msimu mpya wa Bundesliga kwa vishindo.Imetumia Euro milioni 70 kumuajiri staid wa mabingwa wa dunia Itali-Luca Toni,stadi wa makamo-bingwa Ufaransa,Franck Ribery na mshambulizi hatari wa timu ya taifa ya Ujerumani-Miroslav Klose.

Lakini wote hao 3 kumekuwa na shaka-shaka iwapo wataweza kuteremka uwanjani kesho katika mpambano na Hamburg.Wote 3 wameumia.

Kocha wa munich Otmar Hitzfeld huenda ikambidi kumuita Lukas Podolski kuliokoa jahazi.

Schalke 04 ililiangukia mwishoni mwa wiki iliopita ngazi ya 4 ya Ligi,ilifungua dimba la duru hii jana na Bayer Leverkusen.Kusema kweli, Bayern munich yaweza hata kupoteza uongozi wa ligi hii leo ikiwa timu 3 zenye pointi 7 kila moja-Armenia Bielefeld,Bochum na hata Frankfurt zikitamba.

Mabingwa Stuttgart ambao kama werder Bremen walishinda mara ya kwanza mwioshoni mwa juma lililopita tangu kuanza msimu huu,watakuwa uwanjani pia kesho kutimiza miadi yao na Karlsruhe.

Timu nyingi za taifa zitakuwa uwanjani wiki ijayo kwa changamoto za kuania tiketi zao kwa finali za kombe la Ulaya la mataifa 2008 nchini Uswisi.

Kocha wa ujerumani Joachim Loew,amewaita akina miroslav klose,Lukas podolski na Mario Gomez kuongoza hujuma za Ujerumani katika lango la Wales hapo Septemba 8.Nahodha Michael Ballack bado anaugua na hatakuwamo.

Simba wa nyika-Kameroun imemuita mlinzi wao mshahara-Jean-Hugues Ateba kwa changamoto yao ya mwisho ya kugombea tiketi ya kombe la Afrika la mataifa nchini Ghana kati yao na Guinea ya Ekweta hapo septemba 9.Kocha wao Jules Nyongha,hakumteua mshambulizi mpya licha ya kuumia kwa Samuel Eto’o.Eto’o atakua nje ya chaki ya uwanja kwa miezi 2.

Kinyan’ganyiro cha kombe la klabu bingwa barani Afrika kitakuwa pia uwanjani leo na kesho:

Mabingwa Al Ahly ya Misri, wana miadi nyumbani cairo na ASEC Abidjan ya Ivory Coast wakati Esperence ya Tunisia itatoana jasho na Al Hilal ya Sudan iliowazaba mabingwa duru iliopita 3:0.

Alaasiri ya leo itakua zamu ya Al ittihad ya libya kuchuana na Etoile Sportive du Sahel ya Tunisia. Pia FAR rabat ya morocco itakuwa uwanjani na JS Kabylie ya Algeria.

Katika medani ya riadha kwenye ubingwa wa dunia mjini Osaka,Japan, jumla ya medali 5 za dhahabu zinaaniwa :Muethiopia Meseret Defar,ataongoza mkuki wa waethiopia kunyakua medali ya dhahabu katika masafa ya mita 5000.

Tirunesh Dibaba alikwishatoroka na medali ya dhahabu katika mita 10.000.Defa, bingwa wsa Olimpik na wa rekodi ya dunia atasaidiwa na wenzake Meselech Melkamu na Gelete Burika katika jaribio lao la kuzoa medali zote 3.Wakenya,hawatawaachia kuondoka na medali zote.Vivian Cheruiyot wa Kenya, atakua na usemi katika mojawapo wa medali 3.

Macho pia yatakodolewa mbio za mita 100x4 kupokezana ambamo Tyson Gay,anapanga leo kutoroka na medali yake ya 3 ya dhahabu kwa Marekani.Amekwisha shinda mita 100 na 200.