1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BRUSSELS :Umoja wa Ulaya wafikia muafaka wa mkataba mpya

23 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBpG

Wanadiplomasia wa Umoja wa Ulaya katika Mkutano wa Viongozi wa Umoja wa Ulaya mjini Brussels Ubelgiji wamesema viongozi wa nchi wanachama wa umoja huo wamefikia makubaliano na Poland juu ya mkataba mpya wa Umoja wa Ulaya baada ya nchi hiyo kuridhiwa juu ya masuala ya haki za upighaji kura.

Waziri wa Uhispania kwa Umoja wa Ulaya Alberto Navarro amesema kwamba makubaliano hayo yamefuatia mazungumzo kati ya viongozi wa Ufaransa,Uingereza,Ujerumani,Luxembourg na Rais Lech Keczynski wa Poland.

Chini ya makubaliano hayo mapya mfumo wa hivi sasa wa kuzigawanya kura ndani ya umoja huo utaendelea kutumika hadi mwaka 2017.Poland ilitishia kupinga makubaliano ya mkataba huo iwapo kutaanzishwa kwa mfumo mpya wa upigaji kura ambao inadai kuwa ungeliyapa madaraka makubwa zaidi mataifa makubwa ya umoja huo na kuyatia hasarani mataifa madogo ya umoja huo.

Jose Manuel Barroso Rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya amesema kwa kweli wamekuwa wakizungumzia juu ya mageuzi ya asasi za Umoja wa Ulaya kwa takriban miaka saba iliopita na kwamba wakati wa umefika wa kusonga mbele na kuwa ana hisi kuwa wanaweza leo hii kufanikiwa na anaaminini kushindwa hakupaswi kuwa chaguo.

Awali Ujerumani ambayo inashikilia urais wa kupokezana wa umoja huo kila baada ya miezi sita ilitishia kuanzisha mazungumzo mapya juu ya mkataba huo bila ya kuishirikisha Poland.

Mkataba huo unakusudia kuchukuwa nafasi ya katiba ya Umoja wa Ulaya iliokataliwa na wapiga kura wa Ufaransa na Uholanzi miaka miwili iliopita.