1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BEIRUT : Hofu ya umwagaji damu yaongezeka

4 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCmm

Hofu imekuwa ikizidi kuongezeka kwamba maandamano dhidi ya serikali nchini Lebanon yanaweza kugeuka kuwa umwagaji damu wa kimadhehebu baada ya Muislamu wa madhehebu ya Shia kupigwa risasi na kuuwawa katika eneo la Wasunni mjini Beirut.

Duru za usalama zinasema watu wenye silaha waliwafyetulia risasi kundi la waandamanaji waliokuwa wakirudi kutoka kwenye maandamano hayo ya kuipinga serikali katikati ya jiji la Beirut katika kitongoji cha Qasqas chenye Wasunni wengi sana ambayo ni ngome kubwa ya muungano wa kisiasa dhidi ya Syria.

Mwanaume huyo aliepigwa risasi mgongoni alifia hospitalini na watu wenegine 12 walijeruhiwa.Duru za upinzani zinasema shambulio hilo la risasi halitowafanya watelekeze mipango yao ya kuiangusha serikali.

Kundi la Kishia la Hezbollah na washirika wake ambalo linaungwa mkono na Syria na Iran wamepiga kambi kati kati ya jiji la Beirut na wamekuwa wakikesha kucha kutwa kushinkiza kun’gatuka kwa serikali inayoungwa mkono na mataifa ya magharibi ya Waziri Mkuu Fouad Siniora wa madhehebu ya Sunni.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Waarabu Amr Moussa amekutana na viongozi wa Lebanon mjini Beirut na kuelezea wasi wasi wake kwa kusema kwamba nchi za Kiarabu hazistahiki kukaa kando kuangalia mzozo huo ukiripuka.