1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bei ya mafuta imeshuka $67 kwa pipa

Kalyango Siraj24 Oktoba 2008

OPEC yapunguza kiwango cha uzalishaji mafuta kwa siku

https://p.dw.com/p/Fg0L
Bei ya mafuta imeshukaPicha: picture-alliance/ dpa

Mataifa yanayosafirisha nje mafuta kwa wingi duniani ya OPEC yanakutana mjini Geneva leo katika kikao cha dharura ili kutathmini bei ya mafuta.Kufutia kushuka kwa bei ya mafuta barani Asia, mkutano wa OPEC umeamua kupunguza kiwango cha uzalishaji ili bei iweze kupanda.

Bei ya mafuta ilishuka Ijumaa katika bara la Asia.Nchini Marekani alhamisi, bei ya pipa moja ilikuwa chini ya dola 64 .Mwezi Julai pipa moja nchini Marekani lilikuwa linauzwa dola takriban 148.Kushuka kumekuja wakati wa mkutano wa mataifa ya Opec,ambapo umependekeza kupunguza kiwango cha usafirishaji wa mafuta ili kulazimisha bei isiendelea kushuka. Mawaziri wa mafuta wa Opec wamekubali kupunguza uzalishaji wa kiasi cha mapipa millioni moja unusu.Licha ya matarajio hayo lakini bei imeshuka.

Wachambuzi wanatafsiri hali hii kumaanisha kuwa wasiwasi wa kiuchumi umepiku matarajio ya mkutano wa Opec.

Mkutano wa Vienna ulikuwa unatarajiwa kupunguza mafuta kiasi cha mapipa millioni moja kwa siku kama hatua ya kwanza ya kuzuia kushuka kwa bei ya mafuta.Lakini mkutano umekubali kuongeza dau la kupunguza hadi mapipa milioni moja na nusu. Mwanzo kulikuwa na tofauti za kiwango gani kinachofaa kupunguzwa.

Mjumbe mmoja wa Opec kabla ya mkutano aliliambia shirika la habari la Reuters kuwa kundi hilo lilikuwa linatafakari aina mbili ya kupunguza kama suluhisho.Aina ya kwanza ilikuwa kupunguza mapipa millioni moja wa kwa siku leo na kutafakari hali ya mambo hapo baadae katika mkutano utakaofanyika mwezi disemba au kupunguza mapima millioni moja unusu mara moja.Na hilo la pili ndio limepasishwa.

Kabla ya mkutano huo pia Iran,taifa la pili miongoni mwa wanachama wa Opec kwa usafirishaji mafuta kwa wingi,pamoja na Libya zilitaka kila moja kupunguzwe mapipa millioni mbili kwa siku.Hata hivyo Venezuela kwa upande wake ilipendelea kupunguza kwa mapipa millioni moja tu kwa siku.

Saudi Arabia ilikuwa na mawazo tofauti.Waziri wake wa mafuta, Ali al-Naimi, alisema alhamisi kuwa mahitaji ndio yataamua bei ya mafuta na wala sio kupunguza.

Wakati bei ilikuwa juu sana mwezi Julai,Saudi Arabia ilizidisha kiwango chake cha usafirishaji kama jaribio la kupoesha mambo.

Tangu wakati huo Saudi Arabia imepunguza usafirishaji wa mafuta kutokan na na kudorora kwa uchumi kukisababisha mahitaji madogo. Hali hiyo imesababisha kile kinachoweza kuitwa 'mlimbikizo wa mafuta' na bei yake kushuka vibaya,jambo ambalo linafufua kumbukumbuku mbaya kwa Opec za wakati wa mwaka 1998 ambapo bei ya mafuta ilishuka chini ya dola 10 kwa kila pipa.

Hivi majuzi waziri mkuu wa Uingereza,Gordon Brown alisema kuwa upunguzaji wowote wa usafirishaji wa mafuta ambao umechochewa na sababu za kupandisha bei yake,utakuwa kama kashfa hasa wakati huu wa matatizo ya kiuchumi.

Opec huzalisha asili mia 40 ya mafuta yote yanayotumiwa duniani na kiwango chake rasmi cha usafirishaji ni mapipa yanayokaribia millioni 29 kwa siku.Opec ina wanachama 12, ambao ni Algeria, Angola, Ecuador, Iran, Iraq, Kuwait, Libya, Nigeria,Qatar, Saudi Arabia,Umoja wa Falme za Kiarabu pamoja na Venezuela.