1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Beate Zschäpe aomba radhi

9 Desemba 2015

Mtuhumiwa mkuu katika kesi ya mauwaji yaliyofanywa na wafuasi wa chama cha NSU,Beate Zschäpe ameamua hatimae kufumbua mdomo mahakamani.Anadai "hana alichokiona wala kukisikia".Familia za wahanga hawajaridhika.

https://p.dw.com/p/1HKRo
Beate Zschäpe akizungukwa na mawakili wake katika ukumbi wa mahakama mjini MunichPicha: Reuters/M. Dalder

Taarifa kwamba Beate Zschäpe ameamua hatimae kuzungumza zilienea kufumba na kufumbua.Umati wa watu walijazana katika uwanja wa Stigmeier mjini Munich tangu jana usiku.Ndani ya ukumbi wa mahakama,viti vyote 100 vilijaa tangu waandishi habari mpaka watu wa kawaida .Familia za wahanga pia walihudhuria wakijiwekea matumaini pengine Beate Zschäpe angefichua ukweli na pengine kuomba radhi kwa yaliyotokea.

Hakuna kilichotokea.Sio yeye aliyezungumza,bali wakili Mathias Grasel-mmojawapo wa mawakili wawili wepya aliopewa na serikali -huyo ndie aliyesimama kusoma kile alichotaka kukisema Beate Zschäpe mahakamani."Sijahusishwa si katika maandalizi na wala si katika kuyatekeleza mauwaji hayo yaliyofanyika kati ya mwaka 2000 na 2007-amesema Beate Zschäpe katika taarifa hiyo.Hata hivyo anasema anajibebesha jukumu la kiroho kwa kushindwa kuwashawishi washiriki wawili wakati ule ,Uwe Böhnhard na Uwe Mundlos wazuwie mauwaji hayo na ndio maana anasema "anawaomba radhi kwa dhati wahanga wote."

Familia za wahanga hawajaridhika na samaha ya Zschäpe

Binti ya mhanga mmojawapo wa mauwaji hayo amekataa samahani za Beate Zschäpe."Alichokisema Zschäpe hakina maana yoyote" amesema Gamze Kubasikm,binti ya mwenyeduka mmoja aliyeuliwa Dortmund mwaka 2006-Mehmet Kubasik.

Deutschland NSU Prozess
Umati wa watu wanaotaka kusikiliza kesi dhidi ya mwanaharakati wa kundi la siasa kali za amrengo wa kulia- NSUPicha: picture-alliance/dpa/A. Gebert

Mwanaharakati huyo wa zamani wa siasa kali za mrengo wa kulia alijitenganisha na mawakili wake wa awali waliokuwa wakimshauri asiseme kitu mahakamani ili kuepusha asijite matatani.

Beate Zschäpe anafikishwa mahakamani tangu May mwaka 2013 kwa makosa ya kushiriki katika mauwaji ya watu 10,kufanya mashambulio mawili ya mabomu dhidi ya wageni na kuvunja benki mara kumi.

Washiriki wake wawili wakubwa wamefariki dunia

Beate Zschäpe ndie pekee aliyesalimika kati ya kundi la watu watatu,wenzake wawili,Uwe Böhnhardt na Uwe Mundlos walipatikana wameuliwa kwa kupigwa risasi,polisi ilipotaka kwenda kuwakamata mwishoni mwa mwaka 2011 baada ya kuvunja benki moja mashariki ya Ujerumani.

Mathias Grasel NSU Prozess neuer Anwalt Zschäpe
Wakili Matthias Grasel ,mmojawapo wa mawakili wawili wepya wa Beate ZschäpePicha: Reuters/M. Rehle

Wahanga wanane waliouliwa na kundi hilo walikuwa na asili ya kituruki.

Kisa hicho kiliitikisa Ujerumani kwasababu kundi hilo lilikuwa likifanya vituko vyake kwa miaka kadhaa bila ya hofu-hali iliyozusha suala la uzembe katika idara ya upelelezi wa ndani.Mbali na Beate Zschäpe,wafuasi wanne wengine wa wananzi mambo leo wanashitakiwa kwa dhana za kuwasaidia kundi hilo la watu watatu walioishi mafichoni kwa muda wa miaka 13.

Mwandishi: Hamidou Oummilkheir/dpa

Mhariri: Mohammed Khelef