1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern yaishinda Union Berlin kubaki kileleni

Josephat Charo
17 Mei 2020

Mabingwa Bayern Munich walifunga bao la dakika za lala salama katika kipindi cha kwanza na cha pili kuipiku Union Berlin 2-0 katika mechi ya Bundesliga Jumapili (17.05.2020)

https://p.dw.com/p/3cMzz
Deutschland Bundesliga - 1. FC Union Berlin v Bayern München | Robert Lewandowski
Picha: Reuters/H. Hanschke

Bayern sasa wako kileleni mwa msimamo wa ligi na alama 58 wakifuatiwa na Borussia Dortmund katika nafasi ya pili wakiwa na alama 54, baada ya kuicharaza Schalke 4-0 siku ya Jumamosi katika mechi ya watani wa jadi iliyochezwa Signal Iduna Park mjini Dortmund.

Mfungaji bora wa mabao katika Bundesliga, Robert Lewandowski, alifunga penalti dakika ya 40 na Benjamin Pavard akafunga kwa kichwa baada ya kona dakika ya 80 katika uwanja wa Alte Foerstere mjini Berlin ambao haukuwa na mashabiki, na hivyo kuwaweka kifua mbele mabingwa hao kutoka jimboni Bavaria wanaopania kushinda taji la nane mfululizo. Mechi nane zimesalia msimu kukamilika.

Bundesliga imerejea tena kwa masharti magumu mojawapo likiwa suala la mashabiki kutoruhusiwa viwanjani. Polisi wa Berlin walikuwa wamewaonya mashabiki wasifike uwanjani lakini baadhi walikusanyika nje ya uwanja kabla mechi kuanza. Baadaye waliondoka kufuatia mazungumzo na polisi.

(reuters)