1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern Munich na W.Bremen katika finali ya Kombe la DFB leo.

14 Mei 2010

Je, ni Chelsea au Portsmouth itatwaa Kombe la FA ?

https://p.dw.com/p/NOMu
Kombe la DFB- Finali:Olympic StadiumPicha: picture-alliance/dpa/DW

Bayern Munich wanateremka uwanjani Olympic Stadium mjini Berlin hivi punde wakijiwinda kutwaa taji lao la pili msimu huu kabla finali Mei 22 na Inter Milan ya Itali kwa kombe la 3 la champions League.Chelsea nayo yataka pia kuiigiza Bayern Munich leo kutwaa Kombe la FA kwa kuipiga kumbo Portsmouth katika finali ya Kombe hilo.

Kinyan'ganyiro cha Kombe la klabu bingwa kanda ya Afrika mashariki chaanza mjini Kigali,Rwanda-nani ataibuka bingwa mara hii ?Viwanja gani vitachezewa Kombe lijalo la dunia ?

Katika uwanja wa Olimpic stadium Berlin ni finali ya Kombe la Shirikisho la dimba la Ujerumani , jioni ya Jumamosi (leo) kati ya mabingwa wa Ujerumani, Bayern Munich na Werder Bremen, iliomaliza nafasi ya 3 katika ngazi ya Ligi.Kombe litaenda wapi ? Je, Bremen, itaitilia Bayern Munich kitumbua chake mchanga ? Jibu ni baada ya firimbi ya mwisho kulia.

Kinyan'ganyiro cha Kombe la klabu bingwa kanda ya CECAFA-Afrika Mashariki na kati ki naanza leo huko Rwanda.Jumlöa ya timu 11 zinashiriki kuania Kombe hilo la Kagame.Heartland ya Nigeria, imejitoa dakika ya mwisho ,lakini mabingwa wa Afrika TP mazembe wanashiriki.Kenya inawakilishwa na Sofa Paka wakati Tanzania-bara na mabingwa wao Simba huku zanzibar ikitamba na Mafunzo.Msemaji wa CECAFA , Fini Muyestu ameambia Deutsche Welle kuwa matayarisho yote yamekamilika na timu zote zimewasili.

Mexico itakayofungua dimba la Kombe la dunia Juni 11 -wiki kiasi 3 kutoka sasa na wenyeji Afrika kusini au Bafana Bafana, walijiandaa kati ya wiki hii kwa changamoto hiyo kwa kuwalaza majirani wa Afrika Kusini-Angola bao 1:0 mjini Houston,Texas,Marekani mbele ya mashabiki 70.000.

Alikuwa Andres Guardado alielifumania lango la Angola mnamo dakika ya 53 ya mchezo na kutoa salamu kwa Bafana Bafana.

Wenyeji Afrika kusini,ambao walikwisha tangaza kikosi chao cha muda cha wachezaji 29, wameongeza stadi mpya katika listi yao: Bevan Fransman,anaecheza dimba nchini Israel.Mwenyeji huyo wa Cape Town, anaichezea Maccabi Netanya ana umri wa miaka 26. Ameitwa kutokana na kuumia Morgan Gould wa klabu- bingwa SuperSport United.

Miadi ya Bafana Bafana na Mexico Juni, 11, itakuwa katika uwanja wa City Stadium,Johannesberg, katika kitongoji cha Soweto-uwanja unaochukua mashabiki hadi 90.000.

Ikijiandaa kwa changamoto na Mexico, Bafana Bafana kesho Jumapili, inapimana nguvu na Thailand huko Nelspruit kabla kukutana na Bulgaria, Mei 24,Columbia Mei 27 na Denmark Juni 5.

Kuhusu viwanja vitakavyochezewa Kombe la Dunia kati ya Juni 11-Julai 11 vyote vimeshakamilika:

ELLIS PARK:

Huu unachukua mashabiki 61 na ulijengwa 1982.Ulifanyiwa ukarabati kwa Kombe la dunia na ni nyumbani mwa Orlando Pirates.Utachezewa mapambano 5 ya duru ya kwanza, 1 ya duru ya pili na robo-finali.

NELSPRUITni uwanja unaochukua mashabiki 46.000 tu .Huu ulikamilishwa ujenzi mwaka jana na ni mpya kabisa.Utachezewa mapambano 4 ya duru ya kwanza.

POLOKWANE:

Maarufu kwa jina la Peter Mokaba Stadium, uwanja huu, unachukua mashabiki 46.000 na ulikamilishwa ujenzi wake mwaka huu 2010.

PORT ELIZABETH

Au kwa jina jengine : Nelson Mandela Bay Stadium.Uwanja huu unachukua hadi mashabiki 48.000 na ni mpya kabisa ukiwa umemalizika kujengwa mwaka jana.Utachezewa mapambano 5 ya duru ya kwanza ,mpambano 1 wa duru ya pili na robo-finali.

CAPE TOWN:

Uwanja mwengine maridadi ajabu ni ule wa Cape Town unaochukua mashabiki 70.000.Uwanja huu, ulikamilishwa ujenzi mwaka jana ukiwa mpya kabisa na utachezewa mapambano 5 ya duru ya kwanza.Mpambano 1 wa duru ya pili na 1 wa robo-finali.

DURBAN:

Kama huo wa Cape Town, huu unachukua pia mashabiki 70.000 na ni mpya kabisa ukiwa umemalizwa ujenzi wake mwaka jana 2009.Ni uwanja wa klabu ya AmaZulu.Utachezewa mapambano 5 ya duru ya kwanza,1 wa duru ya pili na wa nusu-finali.

Mwandishi:Ramadahan Ali /dpa,rtr,afpe

Mpitiaji:Mohammed Abdul-Rahman