1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ban akosowa sera za kubana wakimbizi Ulaya

Admin.WagnerD28 Aprili 2016

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon akosoa kile alichokiita kuongezeka sera za kuwabana wakimbizi barani Ulaya wakati bara hilo likikabiliana mzozo mbaya kabisa wa wahamiaji kuwahi kushuhudiwa kwa miaka mingi.

https://p.dw.com/p/1IeqO
Picha: picture-alliance/dpa/C. Bruna

Katiba hotuba aliyoitowa katika bunge la Austria Ban amesema anatambuwa ukarimu uliyoonyeshwa hadi sasa na watu na serikali za Ulaya kwa wahamiaji na wakimbizi lakini ana wasi wasi kwamba nchi za Ulaya hivi sasa zinazidi kupitisha sera zenye kuwabana wahamiaji na wakimbizi.

Ban amesema "Sera hizo zinakuwa na taathira mbaya kwa wajibu wa mataifa wanachama kwa sheria ya kimataifa ya ubinaadamu na sheria ya Ulaya.Nakaribisha mjadala wa wazi barani Ulaya ikiwemo Austria kuhusu kujumuishwa kwa wahamiaji katika jamii.Lakini nina wasi wasi tena juu ya kuongezeka kwa chuki dhidi ya wageni."

Kauli hiyo ya Ban inakuja siku moja baada ya bunge la Austria kupitisha mojawapo ya sera kali kabisa za kuomba hifadhi wakati viongozi wa kisiasa wa nchi hiyo wakiwa mbioni kuzuwiya kuibuka kwa wafuasi wa sera kali za mrengo wa kulia ambao wanaongoza katika uchaguzi wa rais.

Sheria tata

Muswada huo wenye utata mkubwa ambao umepitishwa kwa kura 98 dhidi ya 67 unairuhusu serikali kutangaza hali ya hatari iwapo idadi ya wahamiaji inaongezeka kwa ghafla na kukataa takriban waomba hifadhi wote moja kwa moja kutoka mpakani wakiwemo wale kutoka nchi zilizokumbwa na vita kama vile Syria.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon katika bunge la Austria. (28.04.2016)
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon katika bunge la Austria. (28.04.2016)Picha: picture-alliance/dpa/C. Bruna

Iwapo utarattibu huo utaanza maafisa wa mipakani watawaruhusu kuingia tu kwa wakimbizi wanaokabiliwa na vitisho vya usalama katika nchi wanakopitia kwa muda au wale ambao jamaa zao tayari wako nchini Austria.

Makundi wakiwemo watoto wadogo na wanawake wajawazito hawatohusishwa na sheria hiyo.

Hatua hizo ni sawa na zile zilizochukuliwa na serikali ya sera kali za mrengo wa kulia katika nchi jirani ya Hungary mwaka jana.

Wabunge pia wamepiga kura kuzibana sheria za kuomba hifadhi ziliopo hivi sasa kwa kuweka kikomo kwa muda wa hifadhi wanaopatiwa wahamiaji na kufaya iwe vigumu zaidi kwa familia zao kujiunga nao.

Sheria yakosolewa

Vyama vya upinzani na mashirika ya haki za binaadamu vimeshutumu sheria hiyo wakati shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa likionya kwamba linaondowa muhimili wa kuhifadhi wakimbizi.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon katika bunge la Austria. (28.04.2016)
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon katika bunge la Austria. (28.04.2016)Picha: Reuters/K.-H. Bader

(Katibu Mkuu wa Umoja wa Mtaifa Ban Ki-moon pia amewataka viongozi wote wa Ulaya kutekeleza kwa vitendo misingi iliyoiongoza bara hilo na kwamba kuwagawa na kuwatenga watu na kuwamba kunawaumiza watu binafsi na kudhoofisha usalama.

Austria ilipokea waomba hifadhi 90,000 mwaka jana lakini serikali ya mrengo wa wastani inakabiliwa na shinikizo kutoka umma mkubwa unaounga mkono chama cha Uhuru cha mrengo wa kulia.

Zaidi ya watu milioni moja hususan kutoka Syria,Iraq na Afghanistan wamewasili Ulaya mwaka jana na kuchochea mzozo mbaya kabisa wa wahamiaji barani Ulaya kuwahi kushuhudiwa tokea kumalizika kwa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia.

Mwandishi: Mohamed Dahman/AFP/dpa

Mhariri: Iddi Ssessanga