1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Korea Kaskazini yasema mazungumzo na Marekani hayahitajiki.

Tatu Karema
9 Desemba 2019

Balozi wa Korea Kaskazini katika Umoja wa Mataifa amesema mpango wa matumizi ya nyuklia sio wa kujadiliwa tena na Marekani na mazungumzo kati yao hayahitajiki, taarifa inayotilia mkazo tofauti kati ya pande hizo mbili .

https://p.dw.com/p/3UP49
Nordkorea Propaganda l Eröffnung der Musterstadt Samjiyo - Kim Jong Un, Archiv
Picha: Reuters/KCNA

Rais wa Marekani Donald Trump alijaribu kupuuza hatua ya kuongezeka kwa hofu na Korea Kaskazini akisisitiza kile alichosema ni uhusiano mzuri na kiongozi Kim Jong Un na kusema kwamba alifikiria Kim alitaka kuingia katika makubaliano ya kutoingilia uchaguzi mkuu wa urais wa Marekani mwaka ujao.

''Tutaona kuhusu Korea Kaskazini. Nitashangaa iwapo Korea Kaskazini itaonyeshaa uhasama,'' Trump aliwaambia wanahabari katika ikulu ya white house kabla ya kuondoka kuelekea Florida. Trump aliendelea kusema, ''anafahamu nina uchaguzi unaokuja. Sidhani kama anataka kuingilia suala hilo, lakini tusubiri kuona...nadhani anapenda kuona jambo jipya likitokea. Uhusiano ni mzuri sana , lakini unajuwa, kuna uhasama unaoonekana , hakuna swali kuhusu hilo.''

Trump ametumia wakati mwingi kujaribu kuishawishi Korea Kaskazini kufutilia mbali mpango wake wa kinyuklia ambao unaitishia Marekani lakini ni ufanisi mdogo uliopatikana licha ya mikutano yake mitatu na Kim Jong Un.Hofu imeongezeka kabla ya muda wa mwisho wa mwaka mmoja uliowekwa na Korea Kaskazini ambayo imeitaka Marekani kubadilisha sera zake za kusisitiza Korea Kaskazini ifutilie kabisa matumizi ya kinyuklia na kutaka afueni ya vikwazo vya adhabu.

Kim Jong Un ameonya kuhusu,'' hatua mpya'' ambazo hazikutajwa mwaka ujao, na kuzua wasiwasi kwamba hii huenda ikamaanisha kumalizika kwa kuahirishwa kwa matumizi ya mabomu ya kinyuklia na kujaribiwa kwa makombora ya masafa marefu ambayo yamekuwa tangu mwaka 2017 na ambayo Trump ametumia kama ushindi wake katika juhudi za ushiriki.

UN Generalversammlung Rede Kim Song
Kim Song, balozi wa Korea Kaskazini katika Umoja wa MataifaPicha: picture-alliance/dpa/R. Drew

Katika taarifa, Balozi katika Umoja wa Mataifa Kim Song, amesema '' mazungumzo hayo endelevu' yanayoitishwa na Marekani ni, ''njama ya kuokoa wakati,'' kunufaisha agenda yake ya kisiasa nchini Marekani, hii ikimaanisha juhudi ya Trump za kutaka kuchaguliwa tena wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. Amesema kuwa,''hatuhitaji kuwa na mazungumzo marefu na Marekani sasa na mazungumzo kuhusu usitishaji wa matumizi ya nyuklia, hayako tena katika meza ya mjadala na Marekani.''

Matamshi ya Kim Song yanaonekana kuwa na uzito zaidi kuliko onyo la awali la Korea Kaskazini kwamba mazungumzo kuhusiana na mpango wa silaha za nyuklia huenda yakalazimika kuondolewa katika meza ya majadala kutokana na hatua ya Marekani ya kukataa kutoa makubaliano.

Wiki iliyopita, waziri wa mambo ya nje wa Korea Kaskazini alirejelea wito kwa Marekani kubadilisha sera zake kali na kusema kilichobakia ni kwa Marekani kuamua ni zawadi ipi ya Krismasi itapatikana mwishoni mwa mwaka.Kim Song pia alikashifu taarifa kutoka kwa wanachama wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa wa Umoja wa Ulaya iliyoshtumu uzinduzi wa makombora ya masafa mafupi uliotekelezwa na Korea Kaskazini na kuiita'' uchokozi mbaya'' na kusema wanatumiwa na Marekani.

Wajumbe wengi na wachanganuzi pamoja na Marekani, wametilia shaka kwa muda mrefu kujitolea kwa Korea Kaskazini kujadilia mpango wa kinyuklia ambao umetumia raslimali nyingi za serikali na miongo kadhaa ya uwekezaji. Hata hivyo Jenny Town wa 38 Kaskazini, mradi wa Korea Kaskazini mjini Washington, amesema bado haijabainika wazi jinsi matamshi ya Kim Song yanavyopaswa kuchukuliwa. Jenny ameongeza kusema kuwa, uteuzi wa Kim Song kama msemaji ni wa kushangaza kwasababu hahusikii moja kwa moja katika harakati za mazungumzo.