1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika yataka ushirikiano wa usawa baina yake na Ulaya

Sekione Kitojo30 Novemba 2010

Kiongozi wa Libya kanali Moammar Khadafi amesema kuwa Afrika iko tayari kufanya mahusiano na mataifa mengine

https://p.dw.com/p/QLfB
Kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi wakati wa kikao cha mkutano huo.Picha: picture-alliance/dpa

Afrika inapambana ili kupata makubaliano mazuri ya kiuchumi pamoja na umoja wa Ulaya wakati kiongozi wa Libya, Moammer Kadaffi, alipofungua mkutano muhimu kati ya bara la Afrika na Umoja wa Ulaya jana mjini Tripoli Libya, na kutoa onyo kuwa bara la Afrika liko tayari kufanya mahusiano na mataifa mengine.

Akifungua mkutano huo wa kwanza katika muda wa miaka mitatu kati ya mabara hayo mawili, Kanali Ghaddafi aligusa vidonda ambavyo tayari vimekwisha pona kati ya mataifa hayo ambayo ni wakoloni wa zamani na mataifa ya Afrika ambayo yanaadhimisha nusu karne tangu kujipatia uhuru, wakati ambapo jukumu kubwa la hivi sasa ni juhudi za kupatikana ushirikiano mpya ambapo kila upande utakuwa na haki sawa. Katika hotuba yake ya dakika 45 Ghaddafi amesema kuwa Afrika inataka uhusiano wa nipe nikupe ulio katika msingi wa mahusiano ya usawa na sio unyonyaji.

Rais wa umoja wa Ulaya Herman van Rompuy amejibu kwa kusema kuwa uzoefu wa bara la Ulaya katika mwelekeo wa ukuaji wa uchumi unakwenda sambamba na vigezo vya utawala bora.

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani Guido Westerwelle pia amezungumzia umuhimu wa bara la Afrika kwa bara la Ulaya.

Landtagswahl Hessen 2009 Guido Westerwelle
Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani Guido Westerwelle.Picha: AP

Rais wa halmashauri ya umoja wa Ulaya, Jose Manuel Barroso, amesema umoja wa Ulaya ndio hadi sasa mfadhili mkubwa wa msaada wa kibiashara , ikiwa imetoa kwa bara hilo kiasi cha Euro bilioni 10 katika mwaka 2008.

Wakati huo huo, umoja wa Ulaya na mataifa ya bara la Afrika yataitaka Sudan leo kukubali matokeo ya kura ya maoni itakayofanyika mwakani kuamua iwapo upande wa kusini ujitenge, katika taarifa ya pamoja ambavyo imepatikana na vyombo vya habari.

Kura ya maoni itakayofanyika Januari 9 katika eneo hilo ambalo lina utajiri mkubwa wa mafuta inatarajiwa kuamua eneo hilo kuwa huru, wamesema wanadiplomasia na wadadisi wa masuala ya kisiasa, lakini pia inaweza kuwa ni chanzo cha kuzuka tena kwa mzozo .

Wasi wasi juu ya kura hiyo ya maoni , ikiwa ni sehemu ya makubaliano ya amani ya mwaka 2005 ambayo yamemaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe kati ya upande wa kusini na kaskazini , yameelezwa katika taarifa ya pamoja itakayotolewa katika mkutano huo kati ya mataifa hayo ya Umoja wa Ulaya na Afrika nchini Libya hii leo.

Mwandishi Schaeffer ,Utte/ ZR/ Sekione Kitojo

Mhariri: Miraji Othman