1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Yoshihide Suga ateuliwa kuwa waziri mkuu mpya wa Japan

Tatu Karema
16 Septemba 2020

Bunge nchini Japan limemteuwa Yoshihide Suga kuwa waziri wake mkuu na kujaza nafasi iliyoachwa wazi na kiongozi wa muda mrefu Shinzo Abe baada ya kujiuzulu kutokana na sababu za kiafya. Suga ni mshirika wa karibu wa Abe

https://p.dw.com/p/3iXmh
Japan Wahl neuer Regierungschef Yoshihide Suga
Picha: Reuters/K. Kyung-Hoon

Yoshihide Suga aliteuliwa na bunge hii leo na kumfanya kuwa waziri mkuu mpya wa nchi hiyo baada ya muda wa miaka minane wa uongozi wa Abe. Suga ambaye awali alihudumu kama waziri na msemaji mkuu wa serikali, tayari ameunda baraza la mawaziri ambalo limechanganya mawaziri wa kitambo na wale aliowateuwa sasa. Baraza hilo litaandaa kikao chake cha kwanza baadaye hii leo.

Suga mwenye umri wa miaka 71 na mshirika wa karibu wa Abe, ameahidi kuendeleza mipango mingi iliyoanzishwa na Abe inayojumuisha mikakati ya kiuchumi na mageuzi ya kimfumo ikiwa ni pamoja na kuondoa sheria na kufikisha mwisho mizozo ya urasimu. Pia amesema kuwa masuala atakayoyapa kipaumbele ni mapambano dhidi ya virusi vya corona na kufufua uchumi uliodorora kutokana na janga hilo.

Premierminister Shinzo Abe Japan  Ausweitung Maßnahmen Coronavirus
Shinzo Abe- Aliyekuwa waziri mkuu wa Japan Picha: Reuters/T. Ohsumi

Kabla ya uchaguzi wa Suga kuwa rasmi, Abe alisema kuwa kama mwanasheria, ataunga mkono serikali ya Suga na kuwashukuru watu kwa uelewa wao kwa kumuunga mkono Suga.

Suga amepongeza sera za kidiplomasia na kiuchumi za Abe na kusema ataunda taasisi mpya ya serikali kuharakisha mabadiliko ya kidigitali nchini humo ambayo bado yako nyuma. Huku akikosa uzoefu wa moja kwa moja wa masuala ya kidiploamasia, Suga atapaswa kukabiliana na mvutano unaoongezeka kati ya Marekani na China , kubuni ushirikiano na mshindi wa uchaguzi wa Marekani wa Novemba 3 na kujaribu kuweka sawa uhusiano wa Japan na China.

Mwezi uliopita, waziri mkuu anayeondoka Shinzo Abe, alijiuzulu kwasababu za kiafya baada ya kuhudumu kama kiongozi wa nchi hiyo kwa muda wa miaka minane.