1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Tanzania achaguliwa kua naibu katibu mkuu wa Umoja wa mataifa

6 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCct

New-York:

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon amemteuwa waziri wa mambo ya nchi za nje wa Tanzania bibi Asha-Rose Migiro kua naibu wake.Akitangaza habari hizo,katibu mkuu wa Umoja wa mataifa amemtaja mwanadiplomasia huyo wa Tanzania kua kiongozi anaeheshimiwa sana ,anaetetea mataifa yanayoendelea, na stadi anaesifiwa katika shughuli za uongozi.Katibu mkuu Ban Ki-moon amesema anadhamiria kumkabidhi bibi Asha Rose Migiro sehemu kubwa ya shughuli za uongozi na utawala,masuala ya uchumi jamii na maendeleo.

Dr. Asha Rose Migiro mwenye umri wa miaka 50 aliwahi kua mhadhiri mwandamizi katika kitivo cha Sheria cha Chuo kikuu cha Daresalaam,waziri wa maendeleo ya jamii,jinsia na watoto,kabla ya kukabidhiwa wadhifa wa waziri wa mambo ya nchi za nje wa Tanzania,mwezi january mwaka 2006.

Dr. Migiro aliyejipatia shahada ya udaktari wa sheria katika chuo kikuu cha Konstanz nchini Ujerumani ni mwanamke wa pili kushika wadhifa wa naibu katibu mkuu wa Umoja wa mataifa,baada ya Louise Frechette wa Canada.