1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri mkuu wa Uingereza Gordon Brown kulifanyia mabadiliko baraza la mawaziri.

5 Juni 2009

Hadi sasa jumla ya mawaziri wanne wamekwisha jiuzulu.

https://p.dw.com/p/I4E7
Waziri mkuu wa Uingereza Gordon Brown.

Waziri mkuu wa Uingereza, Gordon Brown, analifanyia mabadiliko baraza lake la mawaziri baada mawaziri kadha kujiuzulu na pia baada ya ishara kuwa chama chake cha Labour kilipata matokeo mabaya katika kura ya bunge la Ulaya pamoja na katika uchaguzi wa ndani.

Brown, alipata pigo lingine baada waziri wake wa ulinzi kujiuzulu hii leo baada ya waziri mwingine kujiuzulu na kumtaka pia Brown ajiuzulu

John Hutton ni waziri wa nne kujiujiuzulu baada ya mawaziri Jacqui Smith, Hazel Blears na James Purnell kujiuzulu. Hata hivyo, mawaziri kadha bado wanamuunga mkono Brown, huku, lakini, serikali ikiandamwa na kashfa za matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi miongoni mwa wabunge.

Ninaamini sasa kuwa kuendelea kwa uongozi wako kunakiongezea ushindi chama cha Conservative na hili si jambo zuri kwa nchi yetu, kwa hiyo nakutolea wito ujiuzulu na kukipa chama chetu nafasi ya kushinda, aliandika kwenye barua yake ya kujizulu waziri wa kazi, James Purnell.

Uchaguzi mkuu ni lazima ufanyike mwaka 2010 ambapo chama cha upinzani cha Conservative huenda kikashinda kutokana na kura ya maoni.

Mabadiliko ya leo ya baraza la mawaziri huenda, hata hivyo, yakapelekea mawaziri, wakiwemo waziri wa fedha, Alistair Darling, pamoja na waziri wa masula ya kigeni, David Miliband, wakiendelea kushikilia nyadhifa zao.

Mabadiliko hayo katika baraza la mawaziri yanakuja baada ya kura ya jana Alhamisi ambapo chama cha labour kimepoteza viti 23 huku kile cha upinzani cha Conservative kukijiongezea viti 18 kwenye uchaguzi wa halmashauri za miji.

Matokeo ya uchaguzi wa bunge la Ulaya ambao pia ulifanyika jana, hayatatolewa hadi siku ya jumapili wakati matokeoa hayo yatakapotolewa kutoka nchi sote za bara la Ulaya.

Der britische Arbeitsministers James Purnell
James Purnell, mmoja wa mawaziri waliojiuzulu.Picha: dpa

Kura ya maoni inaonyesha kuwa chama cha labour, kitapata matokeo mabaya zaidi na hata kushika mkia, kikifuata vyama vya conservative, Liberal democrats na hata kile cha United Kingdom Independence.

Hata hivyo, matamshi ya Purnell ya kumtaka Brown ajiuzulu hayakupata uungwaji mkono baada ya mawaziri kadha kufika katika vituo vya radio na runinga kumtetea waziri mkuu Brown.

Ninaendelea kuamini kuwa Gordon Brown ndiye bora zaidi kwa kazi hii, alisema waziri wa afya, Allan Johnson, ambaye pia anakisiwa kuwa anaweza kuchukua mahala pa bwana Brown na kuongeza kuwa huu ndio wakati wa kuungana kwa niaba ya chama na serikali.

Kiongozi wa chama cha Conservative, David Cameron, baada ya ishara kuwa huenda akawa waziri mkuu kwa muda wa mwaka mmoja ujao alisema kuwa kujiuzulu kwa James Purnell kulionyesha kuwa serikali inaendelea kusambaratika na akatoa wito wa kufanyika kwa uchaguzi wa mapema.

Tangu kingie madarakani mwaka 1997 chama cha labour kimekabiliwa na kashfa zikiwemo za matumizi mabaya ya pesa za walipa kodi miongoni mwa wabunge na kuwafanya 17 kati yao kusema kuwa watajiuzulu.

Wakati huo huo, hasira za wananchi zinaendelea kupanda kutokana na kashifa hizo, wakati huu ambapo Uingereza inakabiliwa na hali mbaya ya kiuchumi kuwahi kushuhudiwa tangu vita vikuu vya pili vya dunia.

Vyombo vya habari vanaripoti kuwa kundi la wabunge walioasi linasambaza barua inayomtaka Brown ajiuzulu ambayo wanatarajiwa kumkabidhi baada ya matokeo yote ya kura ya Bunge la Ulaya kutolewa siku ya Jumatatu

Mwandishi : Jason Nyakundi/AFP

Mhariri : Othman Miraji