1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WASHINGTON : Rais Bush ana mashaka kurudisha vikosi

14 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCsn

Rais George W Bush wa Marekani akiwa kwenye shinikizo kutoka kwa wabunge walio wengi bungeni wa chama cha Demokrat kutaka kubadili mwelekeo wake nchini Iraq amepokea kwa mashaka wito wao wa kutaka kurejeshwa kwa awamu wanajeshi wa Marekani kutoka Iraq.

Bush alikutana kwa faragha na wajumbe wa jopo la vyama viwili vikuu vya kisiasa nchini humo ambalo lilikuwa likitarajiwa kumshinikiza abadili mkakati wake nchini Iraq kutokana na kupamba moto kwa umagaji damu,kuongezeka kwa maafa ya Wamarekani na wasi wasi miongoni mwa wananchi wa Marekani kwamba hakuna mwisho ulio karibu wa vita hivyo.

Carl Levin mbunge wa Demokrat wa jimbo la Michigan ambaye atakuwa mwenyekiti wa Kamati ya Huduma za Jeshi ya baraza la Senate hapo mwezi wa Januari amesema inabidi wawapatie Wairaq wenyewe wajibu mkubwa zaidi na njia ya kufanya hivyo ni kuondowa wanajeshi wa Marekani nchini humo kwa awamu.

Hatua ya kuondowa wanajeshi wa Marekani nchini Iraq imepingwa vikali na Rais Bush wakati wa kampeni ya uchaguzi wa bunge na hakuna ishara kwamba atakubali mpango huo hivi sasa.

Wakati akiangalia uwezekano wa kuwa na mkakati mpya kwa Iraq Rais Bush hakupokea kwa shauku ushauri wa washirika wake wa kutaka kushirikishwa kwa Syria na Iran katika suala la kuleta utulivu nchini Iraq.