1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WASHINGTON: Marekani na Umoja wa Ulaya zakubaliana kupambana na ongezeko la joto duniani

1 Mei 2007
https://p.dw.com/p/CC5Z

Marekani na Umoja wa Ulaya zimekubaliana kwamba ongezeko la joto duniani ni swala linalotakiwa kushughulikiwa kwa haraka.

Kansela wa Ujerumaji, Bi Angela Merkel, ambaye nchi yake inashikilia urais wa umoja huo, amesema nchi tajiri duniani zinatakiwa kuongoza juhudi za kupunguza gesi kutoka viwandani ambazo husababisha ongezeko la joto duniani.

Marekani imekuwa ikisita kuweka viwango vya gesi zinazotoka viwandani kwa hofu ya kuvuruga uchumi wake. Lakini kansela Merkel amesema wakati umewadia kwa Marekani kuanza kuchukua hatua.

´Dharura ya kulishughulikia tatizo hili sasa itaonekana pia nchini Marekani, ikiwa bado tunaweza kusema kwamba malengo ya Umoja wa Ulaya ni ya kima cha juu na yanahitaji bidii kubwa kuyafikia.´

Umoja wa Ulaya na Marekani pia zimefikia makubaliano ya kiuchumi yanayolenga kuboresha biashara na kupunguza gharama kwa kuainisha sheria.

Pande hizo pia zimesaini mkataba unaoitwa ´Open Skies´ utakaoziwezesha ndege za nchi za Umoja wa Ulaya kutua katika uwanja wowote wa ndege wa Marekani.

Abiria watanufaika kutokana na bei nafuu za usafiri na kuwa na uwezo wa kuchagua mashirika ya ndege wanayotaka kusafiria.