1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanawake weusi wateseka Latin Amerika na eneo la Carribean

21 Juni 2007

Kuna wanawake kiasi cha 75 millioni wenye asili ya kiafrika katika Amerika ya Kusini na eneo la Carribeanwanaomudu kupata nyadhifa za juu katika ulingo wa siasa au kazi za serikali ni chini ya 50.

https://p.dw.com/p/CHkT

Wanaharakati waliodokeza hayo wanasema wanawake wenye asili ya kiafrika kwenye eneo hilo wamewekwa nyuma katika jamii.

Dorotea Wilson kiongozi wa mtandao wa wanaharakati wa kutetea wanawake wenye asili ya kiafrika kwenye eneo la Carribean na Amerika ya Kusini anasema wanawake weusi wanakabiliwa na hali ngumu inayotokana na ukosefu wa usawa katika eneo hilo. Wanabaguliwa waziwazi kwasababu hata katika maeneo ya kutoa maamuzi hawashirikishwi.

Aidha Wilson anasema wanawake weusi ni lazima watie juhudi kubwa dhidi ya ubaguzi huu na chuki wanayowekewa.

Watu millioni 150 katika eneo la Amerika ya Kusini ambao ni wenye asili ya kiafrika wameshindwa kupata nguvu za kupambana na ubaguzi ambao wamekuwa wakikumbana nao kwa miaka nenda rudi na vile vile hawajapata nafasi za kutosha katika majukumu ya masuala ya kisiasa au serikalini.

Tafauti na wenyeji katika eneo hilo ambao wanafikia idadi ya kiasi cha miliioni 40 wamekuwa katika hali barabara kwenye nchi kama Ecodour na Bolivia ambako wameanza kuwakilishwa kisiasa.

Kwa mujibu wa mtandao wa kutetea maslahi ya wanawake weusi Carribean na Amerika ya Kusini, ni chini ya wanawake 50 pekee walioko kwenye nafasi za kutoa maamuzi ya kisiasa katika eneo zima.

Wanawake wenye asili ya Kiafrika hutumika zaidi kama wafanyikazi wa nyumbani huku utafiti uliofanywa ukionyesha kuwa zaidi ya asilimia 90 ya watu wenye asili ya kiafrika ni maskini na wanaweza tu kupata kazi zilizongumu kabisa na zisizo na mshahara mkubwa na wengi hawana elimu.

Kwa mfano nchini Brazil asilimia 71 ya wanawake weusi wanafanya kazi katika sector isiyo rasmi ya kiuchumi ikilinganishwa na asilimia 65 ya wanaume weusi.asilimia 61 ya wanawake weupe na asilimia 48 ya wanaume weupe.

Imebainika pia nchini Brazil watu wenye asili ya kizungu ni matajiri mara mbili na nusu zaidi kuliko watu weusi.

Huko Colombia asilimia 80 ya watu weusi wanaishi kwenye hali mbaya kabisa ya umaskini wakati nchini Cuba taifa la kisosholisti katika eneo la Carrebean watu wenye asili ya kiafrika wanaishi maisha ya kusikitisha zaidi nyumba zikiwa mbovu na mshahara wa chini kabisa.

Dorotea Wilson anasema hali ni ngumu sana ukiwa mtu mweusi katika eneo hilo na hasa ukiwa ni mwanamke.

Binafsi Wilson anasema amekabiliwa na hali ngumu sana nchini mwake Nicaragua babake akifanya kazi kama mchimba migodi kwa miaka zaidi ya 48 mamake akiwa mke nyumbani akilea wanawe tisa na kwahiyo haikuwa rahisi kwao kutimiza malengo yao maishani lakini walitia bidii na hatimaye wakayashinda madhila.

Akieleza zaidi historia yake hadi kufanikiwa kwake, bibi huyo mtawa na mmishonari mwaka 1975 alijiunga na chama cha Sandinista National Liberation Front FSNL na baadae kujihusisha na harakati za kundi la mlengo wa kushoto ambalo lilimng’oa madarakani Dikteta Anastancio Somoza mwaka 1979.

Katika mwaka huo alifanywa kuwa mwanamke wa kwanza mayor wa Puerto Cabezas na baadae kuchaguliwa mbunge akiwakilisha eneo la pwani ya Carribean.

Hadi sasa amesaliwa kuwa mwanachama wa FSNL ambapo baada ya kupoteza kiti chake cha ubunge katika uchaguzi wa mwaka 1990 alirudi tena madarakani mwaka huu chini ya rais Daniel Ortega.